Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiwa katika picha na Makamu wa Rais wa Afriexim Bank (Global Trade Bank), Bw. Haytham ElMaayergi, baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo Benki hiyo imeonesha utayari wa kuendelea kuisaidia Tanzania kupata fedha za ujenzi wa Reli ya Kisasa-SGR pamoja na kuwekeza kwenye miradi mipya ya sekta ya madini na ujenzi wa mradi mkubwa wa hospitali itakayokuwa na viwango vya dunia vya utoaji huduma za matibabu (African Medical Center of Excellence (AMCE).
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Washington D.C, Marekani)
Na Benny Mwaipaja, Washington D.C
Benki ya Afrika ya Uagizaji na Usafirishaji Nje ya Nchi (African Export-Import Bank-Afreximbank) imesema iko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania kupata fedha za ujenzi wa Reli ya Kisasa-SGR pamoja na kuwekeza kwenye miradi mipya ya sekta ya madini na ujenzi wa mradi mkubwa wa hospitali itakayokuwa na viwango vya dunia vya utoaji huduma za matibabu (African Medical Center of Excellence (AMCE).
Ahadi hiyo imetolewa Jijini Washington D.C, nchini Marekani na Makamu wa Rais wa Afriexim Bank (Global Trade Bank), Bw. Haytham ElMaayergi, alipokutana na kufanya mazungumzo na Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), pembezoni mwa Mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.
Alisema kuwa Tanzania ni mdau wa kimkakati wa Benki hiyo na kwamba iko tayari kushirikiana nayo kutekeleza miradi mbalimbali itakayokubaliwa na pande zote mbili itakayokuwa na tija na inayosisimua ukuaji wa uchumi na maisha ya watanzania.
“Tuko tayari kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania katika mradi wa kununua na kuiongeza thamani dhahabu, kuendelea kutafuta fedha za ujenzi wa Reli ya SGR na tunasubiri kukamilika kwa mchakato wa kuwekeza Kituo kikubwa cha Matibabu ya kibingwa ya kiwango cha kidunia nchini Tanzania” Alisema Bw. Haytham ElMaayergi
Kwa upande wake, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, aliishukuru Afreximbank kwa kuendelea kuisaidia Tanzania, si tu katika kufadhili mradi wa reli ya kisasa ya SGR, bali pia katika kusaidia shughuli za jumla za kibajeti za Serikali, ikiwemo nafasi yake kama ntafutaji wa fedha ‘Mandated Lead Arranger’ katika muamala wa ufadhili wa bajeti wa mwaka wa fedha 2024/25.
Alisema kuwa wakati Serikali ikiendelea kuhamasisha fedha za utekelezaji wa vipande vya sita na saba vya SGR kupitia Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), inatarajia pia Afreximbank kushiriki katika mpango huo kutokana na umuhimu wa mradi huo kwa uchumi wa nchi.
Aliiomba Afreximbank kufungua zaidi dirisha la ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) ili kuwawezesha waendelezaji wa miradi na wakandarasi wakuu kushiriki kikamilifu.
Katika sekta ya afya, alisema kuwa Tanzania iko tayari kuwa mwenyeji wa Kituo cha Afrika cha Ubora wa Huduma za Tiba (Africa Medical Centre of Excellence – AMCE), ambacho kinatarajiwa kuwa nguzo muhimu ya kuimarisha miundombinu ya afya nchini na katika ukanda mzima.
Kwa upande wa nishati ya mafuta, Mhe. Balozi Omar aliipongeza Afreximbank kwa ushirikiano wake na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kuonesha nia ya kusaidia uagizaji wa bidhaa za petroli kwa kipindi cha Mei hadi Julai 2026.
Alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa mpango huo katika kuhakikisha usalama wa nishati nchini.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Juma Malik Akil, Katibu Mkuu na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, Bw. Aboud Hassan Mwinyi, Kaimu Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Rished Bade na Viongozi wengine waandamizi wa Serikali na Taasisi zake.
