Featured Kitaifa

WATANZANIA TUENDELEE KUDUMISHA AMANI-DKT. MWIGULU

Written by Alex Sonna
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameendelea kuwasisitiza Watanzania waendelee kudumisha amani nchini kwa sababu inawawezesha kushiriki katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
“Tuwe makini na watu wanaohamasisha uvunjifu wa amani kwa kuwa wengine walipwa kwa vitendo hivyo. Kama wao wamechagua maisha hayo wasiiuze nchi yetu. “Lazima tulinde amani ya nchi yetu.”
Amesema wanufaika wa kwanza wa amani ni wale wanaoishi katika eneo husika, hivyo hawana budi kuendelea kulinda amani na umoja wa kitaifa ili waendeleze shughuli mbalimbali za maendeleo.
Ameyasema hayo leo (Ijumaa, Aprili 17, 2026) alipozungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Kona ya Mbauda akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Arusha.
Waziri Mkuu amesisitiza hayo mara baada ya kukagua barabara ya Kilombero-Mbauda-Kisongo na Mbauda Losinyai zinazojengwa kwa njia nne pamoja na kuwekewa taa.
Ujenzi wa barabara hizo zenye jumla ya urefu wa kilomita 13 ni miongoni mwa maandalizi ya Mashindano ya Mpira wa Miguu ya Mataifa ya Afrika (AFCON), 2027 ambapo Tanzania ni mwenyeji.
Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema kuwa ujenzi wa barabara hizo unakwenda kuwasaidia wananchi wa Arusha pamoja na Watanzania kwa ujumla.
Waziri Ulega amesema mbali na kurahisisha usafiri na usafirishaji wa watu na mizigo, barabara hizo zinakwenda kuondoa tatizo la mafuriko katika baadhi ya maeneo baada ya kujengwa mitaro mikubwa.
 Pia, Waziri Ulega amesema kila baada ya kilomita moja ya barabara kutawekwa taa ambazo zitawawezesha wananchi wa maeneo hayo kuendelea na shughuli za kiuchumi usiku na mchana.
Amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha shilingi bilioni 27 ambapo kati yake bilioni 17 kwa ajili ya mkandarasi na bilioni 10 fidia kwa waliopisha mradi huo.
Naye, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kutokana na miradi ya maendeleo ya wananchi inayotekelezwa katika jiji hilo.
Waziri Makonda ambaye ni mbunge wa Arusha Mjini ametaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na ujenzi wa barabara za njia nne na uwekaji wa taa ambazo zinakwenda kurahisisha ufanyaji wa biashara.

About the author

Alex Sonna