Na Edward Winchislaus.
WANAWAKE wajasiriamali wa vijijini katika wilaya ya Kondoa, mkoani Dodoma, wameanza kuona mwanga mpya baada ya kupatiwa mitungi ya gesi, hatua inayolenga kuwaondoa kwenye matumizi ya nishati chafu ya kupikia na kulinda afya zao.
Ugawaji huo umefanyika leo Machi 28, 2026 kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), ikiwa ni sehemu ya utaratibu wa USCAF unaofanyika kila mwaka ili kurudisha kwa jamii ( CSR) kwa kugusa makundi mbalimbali yenye uhitaji katika jamii
Akizungumza katika hafla hiyo, mgeni rasmi Ramadhani Hamis, aliyemwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kondoa, amesema hatua hiyo ni muhimu katika kupunguza athari za kiafya zinazotokana na matumizi ya kuni na mkaa, ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zikiathiri afya za wanawake na watoto.
Aidha, ameeleza kuwa halmashauri imekuwa ikiendesha kampeni za uhamasishaji kuhusu matumizi ya nishati safi, na tayari imefanikiwa kugawa majiko ya nishati hiyo mara tatu kwa wanawake wajasiriamali, jambo lililoongeza mwamko na uelewa wa jamii juu ya faida zake.
“Ni muhimu kwa akina mama hawa kuhakikisha wanatumia mitungi hii ipasavyo kwa kuijaza gesi inapoisha badala ya kurudi kwenye matumizi ya nishati chafu,” amesema Ramadhani Hamis, akisisitiza umuhimu wa mabadiliko endelevu ya matumizi ya nishati.
Kwa upande wake, Afisa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa UCSAF, Bi. Celina Mwakabwale, amesema taasisi hiyo inaunga mkono juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha wananchi wanapata na kutumia nishati safi ya kupikia, hasa katika maeneo ya vijijini.
Amebainisha kuwa katika awamu hiyo mitungi 50 imegawiwa kwa wanawake wajasiriamali, huku mingine 50 ikitarajiwa kugawiwa kwa makundi mbalimbali ya kijamii, na kwamba zoezi hilo limekuwa endelevu kwa takribani miaka mitatu sasa likiwa na matokeo chanya yanayoonekana.
Wanawake walionufaika na mpango huo walionesha furaha yao, wakieleza kuwa msaada huo utarahisisha shughuli zao za kila siku na kuboresha afya zao kwa kupunguza moshi unaotokana na kuni na mkaa.
“Nimefurahishwa sana na msaada huu; umetupa nafuu kubwa sisi wanawake ambao tulikuwa tukikumbana na changamoto nyingi kutokana na matumizi ya kuni na mkaa,” amesema Bi. Neema Boniphace kutoka kijiji cha Beleko, akiwakilisha wanufaika wengine.
