Katika dunia iliyokabiliwa na changamoto za mabadiliko ya tabia ya nchi na uharibifu wa mazingira, suala la uhifadhi wa mazingira limeendelea kuwa ajenda muhimu ya kitaifa na kimataifa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan ameendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha mazingira yanatunzwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho ikiwa ni pamoja na kuadhimisha kumbukizi ya siku yake ya kuzaliwa tarehe 27 Januari kwa kupanda miti.
Wizara ya Katiba na Sheria imeenzi maono ya Rais na kuonesha kwa vitendo namna sekta ya Sheria na Katiba inavyoweza kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto za mazingira kwa kushiriki zoezi la upandaji miti lililoongozwa na Naibu Waziri wa Wizara Mhe, Zainab Katimba, Katibu Mkuu wa Wizara Eliakim Maswi,Menejimenti na Watumishi wa Wizara hiyo Mtumba, jijini Dodoma.
Suala la uhifadhi wa mazingira ni suala mtambuka linalohusisha Watumishi wa umma na jamii kwa ujumla kwani mazingira salama ni msingi wa haki za binadamu na ni misingi imara ya usimamizi wa rasilimali za asili.
