Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso,akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 28,2026 katika Mji wa Kiserikali Mtumba jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan katika siku 100 za kipindi cha Uongozi wake katika awamu ya sita.

MSEMAJI Mkuu wa Serikali na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa,akizungumza na waandishi wa habari wakati Waziri wa Maji Mhe.Jumaa Aweso,akizungumza kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan katika siku 100 za kipindi cha Uongozi wake katika awamu ya sita.
Na.Alex Sonna-DODOMA
KATIKA siku 100 za uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, Kupitia Wizara ya Maji, hatua mbalimbali za kimkakati zimechukuliwa kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za maji safi, salama na endelevu kwa wananchi wa mijini na vijijini.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 28,2026 kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, Waziri wa Maji Mhe.Jumaa Aweso,amesema,serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuboresha maisha ya wananchi kupitia uimarishaji wa huduma za msingi, hususan sekta ya maji.
Waziri Aweso amesema kuwa Wizara imenunua dira za maji za malipo kabla 2,271 ambazo zinaendelea kufungwa kwa wateja katika maeneo mbalimbali nchini. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi katika matumizi ya maji, kudhibiti upotevu wa mapato pamoja na kuhakikisha wateja wanapata huduma kulingana na matumizi halisi.
Amesema kuwa ujenzi wa mabwawa ya ukubwa wa kati ya Gidahababieg, Mwambazi na Mwamashindike unaendelea kwa kasi. Mabwawa hayo yanatarajiwa kuwa na uwezo wa kutunza zaidi ya mita za ujazo 1,457,000 za maji na kunufaisha wananchi zaidi ya 1,817,800 pamoja na mifugo zaidi ya 356,400.
“Kukamilika kwa miradi hiyo kutachangia kuimarisha upatikanaji wa maji kwa matumizi ya kijamii na kiuchumi, hususan katika maeneo yanayokabiliwa na changamoto ya upungufu wa maji.”amesema Mhe.Aweso
Aidha amesema kuwa Serikali imeimarisha uhifadhi wa vyanzo vya maji kupitia upandaji wa miti zaidi ya 705,300 katika maeneo mbalimbali nchini. Hatua hiyo inalenga kulinda vyanzo vya maji dhidi ya uharibifu wa mazingira na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Pia Serikali imenunua na kugawa pikipiki 216 kwa Jumuiya za Watoa Huduma za Maji Ngazi ya Jamii (CBWSOs) ili kuimarisha usimamizi wa miradi ya maji vijijini. Aidha, jumla ya shilingi bilioni 198.84 zimelipwa kwa wakandarasi na wataalam washauri wanaotekeleza miradi ya maji nchini, hatua iliyochangia kuharakisha utekelezaji wa miradi hiyo.
Vilevile, Serikali imelipa fidia kwa wananchi waliopisha miradi ya maji, imechimba visima 151 katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na kupata hati safi za miradi mikubwa baada ya ukaguzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), jambo linaloonesha uwajibikaji na usimamizi mzuri wa rasilimali za umma.
Utekelezaji wa Mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji
Serikali imeanza utekelezaji wa Mradi wa Mtandao wa Taifa wa Kusambaza Maji (National Water Grid) unaolenga kutoa maji kutoka vyanzo vya uhakika kama maziwa na mito mikubwa na kuyasambaza kwenda maeneo yenye uhaba wa maji. Kupitia Ziwa Victoria, miradi ya maji katika mikoa ya Musoma, Rorya-Tarime, Bunda, Simiyu, Mwanza, Geita, Chato, Biharamulo na Bukoba inaendelea kutekelezwa huku mingine ikiwa tayari imeanza kutoa huduma.
Aidha, usanifu wa mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda Dodoma kupitia Singida (LVD Project) umekamilika na taratibu za kumpata mkandarasi zinaendelea. Kwa upande wa Ziwa Tanganyika, mtaalam mshauri amepatikana kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa miradi itakayohudumia mikoa ya Kigoma, Katavi, Songwe na Rukwa. Hatua za awali pia zinaendelea kwa Ziwa Nyasa ili kuhudumia mikoa ya Njombe na Ruvuma. Vilevile, usanifu wa miradi ya kutumia maji ya mito mikubwa ya Rufiji na Ruvuma umekamilika, hatua inayofungua fursa kubwa ya upatikanaji wa maji katika mikoa ya Kusini na Pwani.
Miradi ya Maji Iliyokamilika
Katika kipindi cha siku 100, jumla ya miradi 16 ya maji yenye thamani ya shilingi bilioni 16.28 imekamilika katika mikoa mbalimbali ikiwemo Simiyu, Njombe, Iringa, Kilimanjaro, Dodoma, Geita na Tanga. Kukamilika kwa miradi hiyo kumewezesha wananchi zaidi ya 118,400 kupata huduma ya maji safi na salama, hivyo kupunguza umbali wa kutafuta maji na kuboresha maisha yao ya kila siku.
Miradi Inayoendelea na Kuanza Kutoa Huduma
Wizara inaendelea kutekeleza miradi 71 ya maji ambayo baadhi yake tayari imeanza kutoa huduma. Miradi hiyo ina thamani ya shilingi bilioni 142.8 na inatarajiwa kunufaisha wananchi wapatao 2,887,029 itakapokamilika. Miongoni mwa miradi hiyo ni Maboresho ya Miundombinu ya Maji Mtwara Mjini, Mradi wa Nzuguni Awamu ya Kwanza Dodoma, Mradi wa Kigamboni Lot III Dar es Salaam pamoja na Mradi wa Mkinga–Horohoro mkoani Tanga ambao utanufaisha zaidi ya wananchi 57,000.
Malipo ya Awali na Usainishaji wa Mikataba
Serikali imelipa malipo ya awali ya shilingi bilioni 5.99 kwa Mradi wa Maji wa Tunduma wenye thamani ya shilingi bilioni 119. Aidha, mikataba ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya maji na usafi wa mazingira katika miji ya Morogoro na Mwanza imesainiwa, sambamba na mikataba mingine mitano ya miradi ya maji katika mikoa ya Mbeya, Njombe, Geita, Singida na Simiyu.
Mafanikio haya ndani ya kipindi cha siku 100 yanaakisi dhamira ya dhati ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha huduma za maji zinaboreshwa, rasilimali za maji zinalindwa na maendeleo endelevu yanapatikana kwa manufaa ya wananchi wote.