Featured Kitaifa

JAJI MWAMBEGELE AKAGUA VITUO VYA KUPIGIA KURA WILAYA YA TANGANYIKA

Written by Alex Sonna

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele ametembelea na kujionea maandalizi ya ujenzi wa vituo 83 kati ya 90 vya Wapiga Kura vilivyotengwa maalum kwaajili ya wakazi wa zilizokuwa Kata za Ilangu, Ipwaga, Bulamata na Mishamo zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi ambazo zilifutwa na Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya), Sura 287.

Jaji Mwambegele alitembelea eneo hilo la Kata ya Tongwe katika Kitongoji cha Luhafwe leo Oktoba 26, 2025 akiwa ameambatana na Mratibu wa Uchaguzi Mkoa wa Katavi, Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Tanganyika na watendaji wengine wa uchaguzi kuangalia maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani uliopangwa kufanyika Oktoba 29, 2025 nchini kote.

Akizungumza akiwa katika eneo la Mnada wa Kitongoji cha Luhafwe, Jaji Mwambegele alisema Tume ilitangaza kuhamisha baadhi ya vituo nje ya Makazi ya Wakimbizi hivyo amefika na kuangalia maandalizi hayo na Tume imetoa matangazo katika maeneo yaliyofutwa na imeweka vituo maeneo jirani.

Naye Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Tanganyika Bi.Kagemlo Mutagwaba amesema wapiga kura kutoka kata zilizofutwa wamehamasishwa na wameonesha utayari wa kujitokeza kupiga Kura katika maeneo mapya yaliyotengwa.

Watanzania wanataraji kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani Oktoba 29, 2025 huku kauli mbiu ikiwa ni “Kura Yako Haki Yako Jitokeze Kupiga Kura.



About the author

Alex Sonna