Featured Kitaifa

MWENGE WA UHURU WASISITIZA UTUNZAJI WA VYANZO VYA MAJI BONDE LA WAMI RUVU.

Written by mzalendoeditor
NA FARIDA MANGUBE, MOROGORO
Mwenge wa Uhuru mwaka 2023 umesisitiza kuimarishwa kwa usimamizi Katika utekelezaji wa sheria kulinda maeneo ya hifadhi za vyanzo vya maji, ikielezwa kwamba athari za mabadiliko ya tabia nchi zimekuwa zikionekana maeneo mengi zaidi nchini.
Hayo yameelezwa ikiwa ni mwendelezo wa mbio za Mwenge wa uhuru mkoani Morogoro, ukiwa wilayani Mvomero Mwenge wa uhuru umezindua, kuweka jiwe la msingi na kutembelea miradi 8 nyenye thamani ya zaidi ya Bil. 1 zikijumuisha fedha kutoka Serikali kuu, Halmashauri, taasisi za Serikali pamoja na wadau wa maendeleo.
Akizungumza kabla ya kuzindua mradi wa utunzaji wa vyanzo vya maji, mazingira na kuzuia uchafunzi na kuendeleza rasilimali za maji, unatekelezwa chini ya Bodi ya maji Bonde la Wami Ruvu, katika kijiji cha Tangeni Tarafa ya Mlali, kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2023 Abdullah Shaib Kaim amesema kupotea kwa uoto wa asili ni matokeo ya kufanya shughuli za kibinadamu kwenye hifadhi za misitu na vyanzo vya maji kinyume na miongozo ya kisheria hivyo ni vyema wananchi wakaacha tabia hiyo.
Akisoma taarifa ya mradi wa utunzaji wa vyanzo vya maji, mazingira na kuzuia uchafunzi na kuendeleza rasilimali za maji, Afisa rasilimali maji Bodi ya maji bonde la wami ruvu Martin Kasambala amesema madi huo umeghalimu shilingi milioni 13 zikiwa fedha za mfuko wa maji na serikali kuu.
Amesema pamoja na uhifadhi mradi huo pia utawezesha kupatikana kwa maji safi na salama katika Bwawa la mindu na mto Ruvu ambavyo ndio vyanzo vya maji vinavyotegemewa na wakazi wa Manispaa ya Morogoro na miko ya Pwani na Dar es Saalam.
Mwenyekiti wa Halmasauri ya Mvomero Yusuphy Makuwa amesema Halmashauri yake imejipanga katika zoezi la kupanda miti na ipo mbioni kuvuka lengo la Serikali la kila Halmashauri ya Wilaya kupanda miti 1, 500, 000 ambalo ni agizo la Makamu wa Rais Dkt.Philip Mpango.

About the author

mzalendoeditor