Uncategorized

BARRICK NORTH MARA YAJIKITA KAMPENI DHIDI YA VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA KATIKA VIJIJI 11 TARIME

Written by mzalendoeditor
Katika kuadhimisha siku Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia Mgodi wa Barrick North Mara umezindua kampeni ya kuelimisha jamii dhidi ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vijiji 11 vinavyozunguka Mgodi huo.
 
Kampeni hiyo inayoendeshwa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijijini), na wadau wengine inaweza kusaidia kupunguza matukio ya ukatili wa kijinsia wilayani humo.
 
Barrick North Mara inashirikisha timu ya wanasheria kutoka Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), maofisa ustawi wa jamii kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tarime (Vijjini), dawati la jinsia Polisi, viongozi wa dini, wenyeviti na watendji wa vijiji kutoa elimu ya masuala dhidi ya ukatili wa kijinsia.
 
“Tumezindua kampeni ya kupinga ukatili wa kijinsia ambapo tutafikia vijiji 11 vinazunguka mgodi wa Barrick North Mara,” Afisa Mahusiano wa mgodi huo, Zachayo Makobero amesema wakati wa kampeni hiyo iliyofanyika katika Shule ya Sekondari JK Nyerere iliyopo Nyamwaga.
 
Vijiji vilivyo jirani na mgodi huo ambavyo vinafikiwa na kampeni hiyo ni Nyangoto, Kewanja, Mjini Kati, Matongo, Kerende, Nyabichune, Genkuru, Msege, Komarera, Nyakunguru na Nyamwaga.
 
 
“Tunawafikia pia viongozi wa dini, wanafunzi wa kike na wananchi kwa ujumla kwenye mikutano ya hadhara na majumba ya ibada,” Makobero amesema na kuendelea: “Lengo kuu la kampeni hii ni kutoa elimu ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vijiji hivi ukiwemo ukeketaji, lakini pia elimu ya masuala mbalimbali ya kisheria kama vile ardhi na mirathi”,amesema.
 
Kauli mbiu ya kampeni hiyo inasema: “Kataa Ukatili wa Kijinsia – Say no to Gender Based Violence”.
Wananchi na wanafunzi kutoka vijiji vinavyozunguka Mgodi wa North Mara wakifuatilia matukio wakati wa kampeni dhidi ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia inayoendeshwa na Mgodi wa North Mara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali iliyozinduliwa jana ambayo itafanyika katika vijiji 11.

About the author

mzalendoeditor