Featured Kitaifa

WALEZI WA KLABU ZA MAADILI WAASWA KUWA NA MAADILI

Written by mzalendoeditor

KAIMU Katibu Msaidizi Kanda ya Kati –Dodoma  Bi. Modesta Mtui,akizungumza wakati akifungua mafunzo ya maadili kwa walezi wa klabu za maadili kutoka shule mbalimbali za msingi na sekondari   Halmashauri ya Jiji la Dodoma .Kushoto kwake ni  Afisa  uchunguzi  Sekretarieti ya Maadili Bw. Anno Mgani na kulia kwa Kaimu Katibu ni Afisa Uchunguzi Sekretarieti ya Maadili Bi. Philipina Kobelo yaliyofanyika leo Oktoba 28,2022 jijini Dodoma.

…………………..

Kaimu Katibu  Msaidizi Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma  kanda ya kati Dodoma  Bi. Modesta Mtui,amewaasa walezi wa klabu za maadili kuwa na maadili mema katika jamii inayowazunguka.

Hayo ameyasema  leo Oktoba 28,2022 jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya walezi wa klabu za maadili kwa shule za Sekondari na Msingi  katika Halmashauri ya Jiji la  Dodoma .

  Bi. Mtui alisema  kuwa walezi wa klabu za maaadili  wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuwa na maadili mema kwani mtoto anachokiona ndicho atakachokiishi hivyo mwalimu yeyote ni kioo kwa wanafunzi wake “Ni ngumu sana kwa mwalimu ambaye hana  maadili  kumfundisha mwanafunzi  kuwa na maadili  mema na mwanafunzi akaelewa’’’alisema.

Bi. Modesta alisema kuwa  lengo la mafunzo hayo kwa walezi wa klabu hizo  ni kupata uelewa wa pamoja juu ya dhana pana  ya maadili ili walezi hao wa klabu za maadili wawasaidie wanafunzi   kuyaishi  yale wanayofundishwa  jambo litakalowasaidia  kuwa waadilifu toka utotoni hata watakapokua wakubwa.

Bi. Modesta alieleza kuwa   Serikali kupitia Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma  ambacho ndio chombo kikuu cha usimamizi wa maadili ya Viongozi nchini , iliona ni vyema kueneza maadili kwa wanafunzi walioko ngazi mbalimbali za masomo kama vile shule za msingi , sekondari pamoja  na vyuo vikuu  kwa kuanzisha klabu za maadili  ikiaminika kuwa tabia na mienendo mwema kwa binadamu hufundishwa tangu akiwa mdogo na hasa akiwa shuleni au chuoni.

Aidha Bi. Modesta alisema kuwa Lengo la kuanzishwa kwa klabu za maadili  ni  kuwajengea  wanafunzi  na wanavyuo misingi bora ya maadili tangu wakiwa shuleni na vyuoni. Klabu hizo pia zitasaidia kuwatengeneza mabalozi wazuri wa Sekretarieti ya Maadili watakaosaidia kueneza na kuelimisha familia zao kwa ujumla juu ya suala la maadili. Klabu hizo pia zitawasaidia wanafunzi kujitambua na kujipambanua kitabia na kuachana na mienendo isiyofaa.

Akibainisha changamoto wanazokutana nazo walezi  wa klabu za maadili  ambao ni waalimu wa shule mbalimbali Mwalimu Marcus Magwa ambaye ni mlezi wa klabu ya maadili  katika shule ya sekondari  Dodoma  alisema kuwa  kutokana na kukua kwa utandawazi kwa sasa watoto wengi wanapata misukumo ya mienendo mibaya kutoka kwenye mitandao  jambo linalowafanya watoto hao kuona kuwa kuwa na maadili ni ushamba mfano katika suala la mavazi mtoto anaona kuvaa nguo zinazomstiri mwili wake ni jambo lililopitwa na wakati.

Aidha Mwalimu Marcus alitoa wito kwa wazazi kutenga muda wa kukaa na watoto wao  na kufuatilia mienendo yao ili kuweza kubaini mapema  iwapo mtoto ana mienendo isiyofaa ili washirikiane na waalimu kuweza kudhibiti hali hiyo mapema .

Pamoja na hayo Mwalimu Marcus alitoa rai kwa Sekretarieti ya Maadili kuongeza kasi ya kueneza maadili nchini hususan kutoa elimu ya mara kwa mara kwa wanachama wa klabu ya maadili  ili kuendana na kasi ya ukuaji wa utandawazi nchini  ’’ utandawazi una nguvu unakua kwa kasi sana’’ alisema.

Katika mafunzo hayo  walezi wa klabu za maadili  watapata  uelewa  wa  pamoja  juu  ya  shughuli  zinazotekelezwa  na  Sekretarieti  ya  maadili,  majukumu ya Sekretarieti ya Maadili .Katika mafunzo hayo walezi wa klabu za maadili watapata fursa ya  kupitia mwongozo wa kuanzisha na kuendesha klabu za maadili katika shule za msingi, Sekondari na Vyuo vya elimu Tanzania na kutoa maoni yao juu ya namna bora ya  utekelezaji wa mwongozo huo.

KAIMU Katibu Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma  Bi. Modesta Mtui,akizungumza wakati akifungua mafunzo ya maadili kwa walezi wa klabu za maadili kutoka shule mbalimbali za msingi na sekondari   Halmashauri ya Jiji la Dodoma .Kushoto kwake ni  Afisa  uchunguzi  Sekretarieti ya Maadili Bw. Anno Mgani na kulia kwa Kaimu Katibu ni Afisa Uchunguzi Sekretarieti ya Maadili Bi. Philipina Kobelo yaliyofanyika leo Oktoba 28,2022 jijini Dodoma.

KAIMU Katibu Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma  Bi. Modesta Mtui,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua mafunzo ya maadili kwa walezi wa klabu za maadili kutoka shule mbalimbali za msingi na sekondari   Halmashauri ya Jiji la Dodoma yaliyofanyika leo Oktoba 28,2022 jijini Dodoma.

About the author

mzalendoeditor