Featured Kitaifa

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE UWEKEZAJI YARIDHISHWA MIRADI YA TBA

Written by mzalendoeditor

Mwenyekiti wa Kamati Jerry Slaa akiongea na uongozi wa TBA katika moja ya nyumba kwenye mradi wa nyumba 3500 eneo la Nzuguni.

……………………….

Na. Mtemi Renatus Sona – Dodoma
Kamati ya kudumu ya Bunge uwekezaji wa mitaji ya umma imeridhishwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) katika kutekeleza kwa ubunifu miradi ya Serikali, baada ya kufanya ziara ya kutembelea baadhi ya miradi inayotekelezwa na TBA mkoani Dodoma.

Miradi iliyotembelewa ni mradi wa ujenzi wa makao makuu ya Shirika la umeme Tanzania TANESCO ulipo eneo la Medeli, ujenzi wa nyumba 20 za viongozi katika eneo la Kisasa na mradi wa ujenzi nyumba 3500 unaotekelezwa eneo la Nzuguni.
Akizungumza baada ya kuona miradi hiyo, Mwenyekiti wa Kamati, Jerry Slaa amesema Kamati imeridhishwa na utekelezwaji mzuri wa miradi hiyo.
“Kamati ya Bunge imeridhika na kazi iliyofanyika ni kubwa na nzuri, tunachotaka tu ni kuongeza kasi na weledi katika kazi, na sisi kama Kamati wakati wowote tutawasaidia katika kufanikisha kutekeleza miradi yenu” amesisitiza Mwenyekiti Jerry Slaa.
Aidha, Kamati imeipongeza TBA kwa kubuni majengo mazuri na kutekeleza ujenzi kwa viwango bora na wameishauri kuanza kutekeleza miradi yake kwa kushirikiana na Sekta binafsi kwa njia ya ubia.
Awali akifanya wasilisho la miradi mbalimbali inayotekeleza nchini, Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch. Daudi Kondoro, alibainisha kuwa TBA imeendelea kuwa mbunifu katika kutekeleza miradi yake, huku akitolea mfano ubunifu uliofanyika katika ujenzi wa nyumba 20 za viongozi eneo la Kisasa Dodoma.
“Tuliona nyumba za awali zilizopo zina maeneo makubwa, hivyo tukaona ni bora tukate baadhi ya maeneo yake na kupata viwanja vikubwa ambavyo vimetosha sisi kujenga nyumba hizo, hii ni sehemu mojawapo ya ubunifu tunaofanya kama Wakala” anabainisha Mtendaji Kondoro
Mradi mwingine mkubwa ambao Kamati pia imepongeza ni ujenzi wa mji wa Serikali, unaojengwa eneo la Mtumba Jijini Dodoma. Katika mradi huo TBA, imefanya ubunifu wa majengo ya Wizara na Taasisi za Serikali zinazojengwa katika mji huo. Lakini pia inajenga jengo la ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Wajumbe wa Kamati ya Bunge wakiingia moja ya nyumba za viongozi zilizojengwa eneo la Nzuguni

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Mhe. Jerry Slaa akipewa maelezo kuhusu  mradi wa nyumba 20 za viongozi katika eneo la Kisasa na Meneja wa Mradi huo, Mhandisi Imabaraka Shedafa

 Mwenyekiti wa Kamati Jerry Slaa akiongea na uongozi wa TBA katika moja ya nyumba kwenye mradi wa nyumba 3500 eneo la Nzuguni

Wajumbe wa Kamati wakiwa katika moja ya nyumba katika mradi wa nyumba 3500 eneo la Nzuguni

Mwenyekiti wa Kamati Jerry Slaa akizungumza baada ya kumaliza kutembelea miradi ya TBA

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania ((TBA), Arch. Daudi Kondoro akishukuru Kamati kwa kutembelea miradi ya TBA, huku akiahidi kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Kamati hiyo

About the author

mzalendoeditor