Featured Kitaifa

SERIKALI YATOA MAAGIZO KWA RFB, TANROADS, TARURA 

Written by mzalendoeditor

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, akifungua warsha ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoandaliwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara jijini Mwanza, warsha iliyoambatana na uzinduzi wa mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa hali ya barabara.

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya akitoa tuzo kwa moja kati ya wahandisi walioweza kusanifu na kujenga barabara na madaraja kwa kutumia rasilimali zilizopo nchini, kwenye warsha ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoandaliwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara jijini Mwanza.

Washiriki wa warsha ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoandaliwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara jijini Mwanza, wakimsikiliza kwa makini Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya (hayupo pichani), wakati akizindua warsha hiyo.

Washiriki wa warsha ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoandaliwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara jijini Mwanza, wakimshangilia Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya (hayupo pichani), wakati akizindua warsha hiyo.

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, akiwa kwenye picha ya pamoja na washindi wa tuzo za kusanifu na kujenga barabara na madaraja kwa kutumia rasilimali zilizopo nchini (waliosimama), kwenye warsha ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoandaliwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara jijini Mwanza

Picha na WUU

……………………………………..

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi sekta ya Ujenzi Mhandisi Godfrey Kasekenya, ameziagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) kuzifanyia kazi kwa wakati taarifa zitakazotolewa na watumiaji wa barabara kupitia mfumo mpya wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa hali ya barabara.

Pia ameiagiza Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB) kufuatilia na kuhakikisha kuwa taarifa na malalamiko yanayoletwa na watumiaji wa barabara yanafanyiwa kazi kwa wakati na Wakala wa Barabara.

Naibu Waziri Kasekenya ametoa maagizo hayo wakati akifungua warsha ya siku mbili ya kujadili namna ya kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi kwenye miundombinu ya barabara, iliyoambatana na uzinduzi wa mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa hali barabara, iliyofanyika jijini Mwanza.

Ambapo ameeleza kuwa ameziagiza TANROADS na TARURA kuzifanyia kazi kwa wakati taarifa zinazoletwa kwao na watumiaji wa barabara kwa lengo la utekelezaji.

“Upatikanaji wa taarifa za hali ya barabara kwa wakati, ni moja ya njia muhimu za kutunza miundombinu ya barabara, naipongeza Bodi ya Mfuko wa Barabara kwa kubuni mfumo wa kielektroniki utakaotumiwa na wananchi na watumia barabara kufuatilia na kutoa taarifa kwa vyombo husika juu ya hali ya barabara katika maeneo yao,”ameeleza Kasekenya.

Pia ameendelea kwa kuziagiza TANROADS na TARURA kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye madaraja na makalavati ili kuepuka kutokea kwa majanga makubwa kama lile la Kiyegeya.

Aidha amezitaka kuingia mikataba ya muda mrefu ya matengenezo ya kawaida ya barabara ili kuziba mashimo yanayotokea barabarani ndani ya saa 48 kwa mujibu wa makubaliano kati ya Bodi na Wakala wa Barabara.

“Nawaagiza TANROADS na TARURA kwa kushirikiana na Bodi, kubainisha kwa wakati maeneo hatarishi ya barabara ambayo huathiriwa na mvua mara kwa mara na kuchukuwa hatua stahiki pamoja na kukamilisha manunuzi ya kazi za matengenezo ya barabara kwa wakati kabla ya majira ya mvua na kuzitekeleza kikamilifu,”ameeleza Kasekenya.

Kwa upande wake Meneja wa Mfuko wa Barabara Eliud Nyauhenga, ameeleza kuwa kwa zaidi ya kipindi cha miaka 20 iliyopita wameshuhudia uharibifu mkubwa wa mara kwa mara wa miundombinu ya barabara kutokana na mafuriko yanayosababishwa na mvua kubwa kupita kiasi zinazosababishwa na mabadiliko ya tabianchi. 

Uharibifu huo ni pamoja na kusombwa kwa madaraja na makalavati kunakoleta usumbufu na hasara kubwa kwa wasafiri na wasafirishaji na kusababisha gharama kubwa kwa Serikali.   

“Mfano wa karibuni ni kuzolewa kwa daraja la Kiyegeya mwaka 2020 ambako kulisimamisha kwa muda shughuli za usafiri na usafirishaji kupitia barabara ya Morogoro – Dodoma ambayo inatumiwa na mikoa ya kati, Kanda ya Ziwa na nchi jirani kama Rwanda, DRC Congo na Burundi, kutokana na kusombwa kwa daraja hilo, Serikali ililazimika kutumia takribani bilioni 10.89 kujenga daraja jipya na barabara unganishi,” ameeleza Nyauhenga.

Ameeleza kuwa pamoja na ufuatiliaji wa kila siku bodi kila mwaka hufanya tathmini ya utendaji wa wakala za barabara kupitia wataalamu elekezi kwa kutumia mfumo wa kutathimini kazi za barabara kwa kuzingatia thamani ya fedha. 

Ambapo vigezo vinavyotumika kufanya tathmini ya utendaji ni umakini katika maandalizi ya mradi, usanifu wa mradi, taratibu za manunuzi, ujenzi au matengenezo ya mradi na kufunga mradi (project closure).

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB) Joseph Haule, ameeleza kuwa sekta ya barabara ni nyenzo muhimu kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

“Bila usafiri wa uhakika wa barabara, ni vigumu wananchi kunufaika na huduma za kijamii na kiuchumi ambazo zinatolewa na kuwezeshwa na Serikali ikiwemo elimu, afya na upatikanaji wa masoko,”ameeleza Haule.

Ameeleza kuwa, miundombinu hiyo inakabiliwa na changamoto zitokanazo na mabadiliko ya tabia ya nchi katika nchi mbalimbali duniani, kama vile mvua kubwa, joto kali, upepo mkali pamoja na kuzidishwa kwa uzito wa magari barabarani.

Takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2020 thamani ya mtandao wa barabara zilizorasimishwa ni  trilioni 21 sawa na asilimia 16 ya pato la taifa.

Akitoa salamu za shukrani, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB) Octavian Mshiu, ameeleza kuwa bodi hiyo itahakikisha kwamba wanasimamia utekelezaji wa maelekezo yote yaliotolewa na Naibu Waziri huyo kwa ukamilifu na kwa weledi wa hali ya juu.  

About the author

mzalendoeditor