Featured Kitaifa

TANZANIA YAPOKEA KWA HESHIMA UONGOZI WA KAMATI YA UHAMIAJI SALAMA WA NGUVU KAZI

Written by Alex Sonna

Na.Alex Sonna, Dodoma

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, amesema Tanzania imepokea kwa heshima jukumu la kuongoza Kamati ya Kikanda ya Ushauri wa Kitaalamu kuhusu Uhamiaji Salama wa Nguvu Kazi, huku akiahidi kutumia nafasi hiyo kushughulikia changamoto zinazowakabili wafanyakazi wanaohamia nje ya nchi.

Sangu ameyasema hayo wakati wa mkutano wa kikanda kuhusu uhamiaji salama wa nguvu kazi, ambapo Tanzania imekabidhiwa uongozi wa kamati hiyo kutoka Uganda. Amesema Serikali imejipanga kuendeleza mazuri yaliyofanywa na Uganda na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizojitokeza kupitia ushirikiano wa nchi wanachama.

Ameipongeza Serikali ya Uganda kwa kazi nzuri iliyofanya wakati wa uongozi wake, akisema Tanzania itazingatia changamoto na mapendekezo yaliyotolewa ili kuimarisha utendaji wa kamati hiyo.

“Tunafikisha salamu zetu kwa uongozi wa Uganda ambao wamefanya kazi nzuri na tunawapongeza sana. Changamoto mlizozitaja mlizokutana nazo tutaendelea kuziangalia kama wenyeviti na wawakilishi wa mawaziri kwa niaba ya Tanzania,” amesema Sangu.

Amesema yuko tayari kukabiliana na changamoto hizo na kuzigeuza kuwa fursa za kuboresha utendaji wa kamati, ili iweze kutimiza malengo yaliyowekwa na kuhakikisha masuala ya uhamiaji salama wa nguvu kazi yanapatiwa ufumbuzi wa pamoja.

Kwa mujibu wa Sangu, uhamiaji wa nguvu kazi una mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo ni muhimu kwa nchi wanachama kuimarisha ushirikiano katika kuhakikisha wafanyakazi wanaohamia nje wanapata mazingira salama na yenye staha.

“Masuala ya uhamiaji yana mchango mkubwa katika maendeleo, lakini tunakutana pia na changamoto ikiwemo kutokueleweka kwa baadhi ya masuala ya unyanyasaji wa wafanyakazi katika maeneo wanayokwenda kufanya kazi,” amesema.

Amesema changamoto hizo zinapaswa kujadiliwa na kutafutiwa ufumbuzi kwa pamoja badala ya kuachiwa nchi moja, huku akisisitiza Tanzania itaendelea kusimamia ajira zenye staha na kuongeza ulinzi kwa wahamiaji, hususan wanawake, wanaokwenda kutafuta fursa za ajira nje ya nchi.

Sangu amesema mafanikio ya uenyekiti wa Tanzania hayatapimwa kwa idadi ya mikutano itakayofanyika, bali kwa utekelezaji wa maamuzi, mikakati na makubaliano yatakayofikiwa na nchi wanachama.

Amesema Tanzania itaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kikanda kuhusu uhamiaji wa nguvu kazi, ikiwemo ajenda za Afrika Mashariki na mipango mingine ya maendeleo inayolenga kuongeza fursa za ajira na kulinda haki za wafanyakazi.

‎Kwa upande wake, Waziri wa Jinsia, Kazi na Maendeleo ya Jamii Uganda, Mhe. Luteni Jenerali Henry Tumukunde amesema ushirikiano wa nchi za Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika katika suala la uhamaji salama wa nguvu kazi utasaidia kuwa na sauti moja katika kutetea haki za wafanyakazi wanaokwenda nje ya nchi.

 Luteni Jenerali Tumukunde amesema nchi za Afrika hazilengi kuwanyanyasa wafanyakazi wanaokwenda nje ya nchi, bali zinapaswa kuwawezesha kutumia fursa zilizopo katika kutafuta ajira na kuboresha maisha yao.

Amesema baadhi ya maeneo yanaweza kuutazama uhamiaji wa nguvu kazi kama njia ya kupata wafanyakazi kwa gharama nafuu, lakini nchi za Afrika zina wajibu wa kuhakikisha haki, usalama na maslahi ya wafanyakazi hao yanalindwa.

 Luteni Jenerali Tumukunde amesema Uganda ina imani kuwa Tanzania itatoa uongozi wenye ujasiri na wenye kuleta matokeo katika jukwaa hilo, ikiwemo kusaidia kutengeneza na kuimarisha sera zitakazowanufaisha vijana wanaotafuta fursa za ajira nje ya nchi.

Amesema changamoto kubwa iliyopo ni kuhakikisha vijana wanaopata fursa za kufanya kazi nje ya nchi wanapata ulinzi unaostahili pamoja na mazingira bora na salama ya kazi.

Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania, Uganda na nchi nyingine za Afrika Mashariki ni muhimu katika kujenga mifumo imara itakayowezesha uhamiaji salama wa nguvu kazi na kuhakikisha fursa hizo zinakuwa na manufaa kwa wananchi na nchi zao.

Naye Mtendaji Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamaji (IOM), Amy Pope amesema Shirika hilo lipo tayari kushirikiana na nchi za ukanda huo ili kuwajengea uwezo nguvu kazi hususani vijana wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi ili wawe na ujuzi unaohitajika.

About the author

Alex Sonna