Featured Kitaifa

WRRB, MIKOA NA HALMASHAURI KUIMARISHA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA

Written by Alex Sonna

Na.Mwandishi Wetu-DODOMA

BODI ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imesema itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri nchini ili kuimarisha utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRS), kuongeza tija kwa wakulima na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, ameyasema hayo leo Agosti 18, 2026, wakati akizungumza na Maafisa Biashara katika Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Bw. Bangu amesema utekelezaji wenye tija wa mfumo huo katika mikoa na halmashauri unahitaji ushiriki wa karibu wa Maafisa Biashara, hususan katika usimamizi wa shughuli zinazohusiana na maghala pamoja na minada ya mazao inayofanyika katika maeneo yao.

Amesema Maafisa Biashara wana nafasi muhimu katika kuhakikisha taarifa sahihi kuhusu mahitaji ya maghala katika maeneo yao zinapatikana, sambamba na kufuatilia hali, matumizi na uhitaji wa maghala katika halmashauri na mikoa ili kuwezesha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutekelezwa kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano wa WRRB, Bw. Dionis Musseru, amesema utoaji wa elimu kwa umma umeendelea kuongeza uelewa na ushiriki wa wadau katika mfumo huo, ambapo hadi sasa mazao 11 yanauzwa kupitia WRS.

About the author

Alex Sonna