Na Alex Sonna, DODOMA
Serikali imezindua Kituo cha Usaidizi wa Upatikanaji wa Vifaa/Bidhaa na Mauzo ya Nje chenye lengo la kuwawezesha wajasiriamali wadogo, vijana na wawekezaji kupata fursa zaidi za kukuza biashara zao na kuingia katika masoko ya kimataifa.
Akiwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, amesema kituo hicho kimeanzishwa kama sehemu ya mkakati wa kuimarisha mazingira ya biashara, kuongeza uzalishaji wa ndani na kuchochea ukuaji wa uchumi unaoshirikisha wananchi wengi.
“Kituo hiki kimeanzishwa ili kuwawezesha wajasiriamali, vijana na wawekezaji kupata huduma muhimu zitakazowasaidia kukuza biashara zao, kuongeza uzalishaji na kufikia masoko mapya ya ndani na nje ya nchi,” amesema Waziri Omar.
Kituo hicho kinatarajiwa kuwa daraja muhimu kwa wajasiriamali na wawekezaji wanaokabiliwa na changamoto za upatikanaji wa mitaji, masoko na vifaa muhimu vya uzalishaji.
Mbali na kusaidia upatikanaji wa mitaji ya biashara, kituo hicho pia kitawaunganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya nje ili kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika soko la kimataifa na kukuza mapato ya fedha za kigeni.
“Wajasiriamali wengi wamekuwa wakikabiliwa na changamoto za kupata masoko ya uhakika na mitaji. Kupitia kituo hiki, serikali inalenga kufungua fursa zaidi za biashara na kuongeza ushiriki wa Watanzania katika biashara za kimataifa,” amesema.
Serikali imeeleza kuwa kituo hicho kitakuwa na jukumu la kurahisisha taratibu za usafirishaji wa mizigo kuingia na kutoka nchini, hatua inayotarajiwa kupunguza gharama za biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko mbalimbali.
Aidha, kituo hicho kitasaidia upatikanaji wa malighafi, mashine na vifaa muhimu vinavyohitajika katika uzalishaji, jambo litakaloongeza uwezo wa viwanda vidogo na vya kati kuzalisha kwa tija zaidi.
“Kupatikana kwa malighafi, mashine na vifaa kwa urahisi kutasaidia kuongeza uzalishaji, ajira na mchango wa sekta binafsi katika ukuaji wa uchumi wa taifa,” amesema Waziri Omar.
Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda unaotegemea ubunifu, uwekezaji na ushiriki mkubwa wa sekta binafsi, huku vijana na wajasiriamali wakitajwa kuwa miongoni mwa wanufaika wakuu wa mpango huo.