Featured Kitaifa

SERIKALI YASISITIZA UENDELEVU WA MABORESHO YA ELIMU YA UALIMU BAADA YA MRADI WA TESP

Written by Alex Sonna

Naibu Katibu Mkuu Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu,Prof Daniel Mushi,akizungumza  wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau wa  TESP na kuhitimisha mradi huo uliofanyika leo Aprili 9,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo.

Na.Alex Sonna-Mzalendo blog-DODOMA

SERIKALI imesisitiza umuhimu wa kuendeleza mafanikio yaliyopatikana kupitia Mradi wa Kusaidia Elimu ya Ualimu (TESP), ili kuhakikisha ubora wa elimu unaimarika kwa vizazi vijavyo.

Hayo yameelezwa  na Naibu Katibu Mkuu Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu,Prof Daniel Mushi, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau wa  TESP na kuhitimisha mradi huo uliofanyika leo Aprili 9,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo.

Amesema kikao hicho si tu hitimisho la mradi, bali ni fursa ya kufanya tathmini, kujifunza na kuweka mikakati ya kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana yanaendelea kudumishwa na kupanuliwa.
Kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Prof. Mushi ameishukuru Serikali ya Canada kupitia taasisi ya Global Affairs Canada kwa ushirikiano na msaada wao uliochangia kuimarisha mifumo ya elimu ya ualimu nchini.
Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa mradi huo mwaka 2017, kumekuwa na maboresho makubwa ikiwemo usambazaji wa zaidi ya vitabu laki moja tisini na sita katika vyuo 35 vya ualimu pamoja na kuunganishwa kwa taasisi hizo na mtandao wa maktaba za vyuo vikuu nchini.
Aidha, zaidi ya vifaa 1,400 vya TEHAMA vimesambazwa, hatua iliyosaidia kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, huku miundombinu kama maktaba na maabara ikijengwa na kukarabatiwa.
Katika hatua nyingine, zaidi ya wakufunzi 1,300 wamepatiwa mafunzo ya mbinu za kisasa za ufundishaji, elimu jumuishi pamoja na matumizi ya teknolojia, huku takribani walimu wanafunzi 73,000 wakihitimu katika kipindi cha mradi huo.
Prof. Mushi amesema mafanikio hayo ni uwekezaji mkubwa katika mustakabali wa elimu nchini, lakini akasisitiza kuwa ni muhimu sasa kuhakikisha yanaendelezwa kupitia ufadhili endelevu, uongozi imara wa taasisi na matumizi sahihi ya rasilimali zilizopo.
Ametoa wito kwa washiriki wa kikao hicho kuweka mikakati madhubuti ya kuendeleza miradi hiyo, kupanua mafanikio yake katika taasisi nyingine na kuimarisha ushirikiano kati ya wizara, taasisi na wadau wa maendeleo.
Ametangaza rasmi kufunguliwa kwa kikao hicho huku akisisitiza kuwa jukumu lililopo sasa ni kuhakikisha mafanikio hayo yanaendelea kuleta matokeo chanya kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Ualimu Tabora, Bi. Balbina Joseph, amesema kuwa Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Ualimu (Teachers Education Support Program – TESP), umeleta maboresho makubwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo utunzaji wa mazingira, usawa wa kijinsia, ujumuishi na upatikanaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Ameongeza kuwa wakufunzi, watumishi na bodi za vyuo wamepata mafunzo yaliyoongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Naye Kaimu Mkuu wa Chuo cha Ualimu Kabanga, Bw. Phonce Mashibe, amesema chuo hicho kimenufaika kwa kiasi kikubwa kupitia ujenzi upya wa miundombinu na uwekezaji katika mifumo ya nishati mbadala. Amefafanua kuwa matumizi ya biogas na nishati ya jua yamepunguza gharama za uendeshaji kwa kiasi kikubwa, zikishuka hadi asilimia 60.

Kwa upande wa wanafunzi, Marry Faustine Igulu, mwanafunzi wa Chuo cha Ualimu Bustani ngazi ya diploma, amesema kuwa  Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Ualimu (Teachers Education Support Program – TESP),umeboresha kwa kiwango kikubwa mazingira ya kujifunzia, ikiwemo ujenzi wa maabara za sayansi, ukarabati wa mabweni, madarasa na maktaba. Ameongeza kuwa upatikanaji wa vifaa vya TEHAMA umeongeza uwezo wa walimu tarajali kutumia teknolojia katika ufundishaji, hatua inayochangia kuinua ubora wa elimu nchini.

About the author

Alex Sonna