Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.
…..
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayetumia kivuli cha uanaharakati kueneza vurugu, kuharibu mali au kuhatarisha usalama wa taifa, akisisitiza kuwa amani ya nchi ni jambo lisilo na mjadala.
Akizungumza Julai 9, 2026 katika Ikulu ya Zanzibar wakati wa hafla ya utiaji saini wa Tamko la Maridhiano kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT Wazalendo, Rais Samia amesema Tanzania itaendelea kulinda amani yake kwa kutumia sheria dhidi ya watu wote watakaojihusisha na vitendo vinavyoashiria ugaidi au kuvuruga utulivu wa nchi.
Amesema kumekuwepo na watu wanaojificha nyuma ya jina la uanaharakati huku wakihamasisha vurugu, kufanya uharibifu wa miundombinu na mali za umma pamoja na kutaka kuishinikiza Serikali kupitia njia zisizo halali.
“Nataka niwaonye wale wote wanaojiita wanaharakati, lakini matendo yao yanaathiri amani ya nchi kwa kujihusisha na vurugu, uharibifu wa mali na miundombinu kwa lengo la kutimiza ajenda zao za kisiasa au kiitikadi,” amesema Rais Samia
Rais Samia amesisitiza kuwa uzalendo wa kweli hauonyeshwi kwa kuichafua au kuiharibu nchi, bali kwa kulinda amani, kuheshimu sheria na kushiriki katika kujenga maendeleo.
Amewakumbusha kuwa hata pale viongozi walipokuwa na tofauti za kisiasa, walichagua njia ya mazungumzo badala ya migogoro na machafuko, jambo lililowezesha Tanzania kuendelea kuwa kisiwa cha amani.
“Aneyeipenda nchi yake hawezi kuiweka katika mazingira ya vurugu. Tofauti zetu zinapaswa kutatuliwa kwa mazungumzo na kuheshimiana, si kwa vitisho wala uharibifu,” amesema
Akizungumzia maridhiano yaliyofikiwa kati ya CCM na ACT Wazalendo, Rais Samia amesema hatua hiyo ni ushahidi kwamba tofauti za kisiasa zinaweza kutatuliwa kwa njia ya mazungumzo na maridhiano badala ya migogoro.
Aidha, amewahakikishia Watanzania kuwa vyombo vya dola vitaendelea kutekeleza wajibu wake wa kulinda usalama wa wananchi na mali zao bila kuyumba.
“Taifa lolote linalojali usalama wa watu wake hutumia mamlaka ya kisheria kulinda amani na heshima yake. Tanzania itaendelea kufanya hivyo bila kusita,” amesema
Hata hivyo Rais Samia amewataka viongozi wa kisiasa na wananchi kuendelea kudumisha mshikamano, akieleza kuwa amani ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa na urithi muhimu kwa vizazi vijavyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na viongozi mbalimbali kwenye hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa kwenye picha na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman baada ya kushuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi kufuatia Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.

Viongozi pamoja na wageni mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi katika viwanja vya Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026.