Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani mkubwa.
Ridhiwani alitoa wito, wakati akizungumza katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Alisema mafanikio ya taaluma katika dunia ya sasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuwa na uwezo wa kushindana nje ya mipaka ya nchi zao huku wakizingatia maadili ya kazi, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri katika fani zao.
“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kuelewa kuwa taaluma zao zinahitaji siyo tu maarifa ya kisheria, bali pia maadili, nidhamu na uzalendo vitakavyowasaidia kuwa wataalamu wenye ushindani na mchango chanya kwa taifa,” alisema.
Aidha, Ridhiwani aliwaeleza wanafunzi hao kuhusu hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha sekta ya sheria na utoaji wa haki nchini.
Alisema serikali imeendelea kufanya mageuzi mbalimbali ikiwemo kuboresha mfumo wa haki, kuongeza matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria, kuwekeza katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.
Kwa mujibu wa Ridhiwani, maboresho hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na wasimamizi wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, sambamba na kujenga mazingira bora ya utoaji haki nchini.
Alisisitiza kuwa sekta imara ya sheria na haki ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku wataalamu wa sheria wakibeba jukumu kubwa la kulinda maslahi ya taifa na kuimarisha utawala bora.



