Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu akizingumza katika Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani ( ILO), Juzi Juni 5, 2026, Jijini Geneva, Uswisi.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu na Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa Nchini Uswisi, Mhe. Dkt. Abdallah Possi wakiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Mkutano Mkuu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), leo Juni 5, 2026, Jijini Geneva, Uswisi.
Na: OWM (KAM) – Geneva, Uswisi
Tanzania imekuwa mwanachama wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) tangu mwaka 1962 na imeendelea kushiriki kikamilifu katika juhudi za kimataifa za kulinda haki za wafanyakazi na kukuza ajira zenye staha. Pia, Tanzania ni mjumbe wa Bodi ya Magavana ya ILO (Governing Body), ikiwakilisha nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki ambapo kupitia nafasi hii imekuwa ikichangia kwa dhati katika maamuzi ya kimataifa yanayohusu Sera za ajira, Haki za Wafanyakazi na Maendeleo ya kijamii, hivyo kuimarisha taswira yake kama mshirika muhimu katika kukuza kazi za staha na usawa katika sekta ya kazi ulimwenguni.
Kupitia Shirika hilo la ILO, kila mwaka imekuwa ikifanyika mikutano ambayo huwakutanisha wawakilishi wa Serikali, Waajiri na Wafanyakazi kutoka katika nchi wanachama 187 kwa lengo la kupanga na kuweka mikakati inayolenga kuboresha na kukuza ustawi wa Sekta ya Kazi Duniani.
Aidha, katika mwaka 2026 Tanzania ni miongoni mwa nchi inayoshiriki katika Mkutano Mkuu wa 114 wa ILO unaofanyika jijini Geneva, nchini Uswisi. Ujumbe wa Serikali ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliongozwa na Waziri wa Nchi anayeshughulikia masuala ya Kazi, Ajira na Mahusiano Mheshimiwa Deus Clement Sangu ambaye mnamo tarehe 5 Juni, 2026 alieleza mambo sita makubwa ambayo Tanzania imeendelea kuyatekeleza katika kuimarisha sekta ya kazi, ajira na ustawi wa wafanyakazi, hatua zinazoiwezesha nchi kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia duniani.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Waziri Sangu ametaja mambo hayo ni pamoja na dhamira ya Tanzania chini ya uongozi wa Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha mabadiliko ya kiteknolojia yanakuza kazi zenye staha, tija, ubunifu na haki ya kijamii kupitia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Pia amesema Tanzania imeendelea kulinda haki za wafanyakazi katika mazingira ya kidijitali kupitia uzinduzi wa Mpango wa Taifa wa Kazi Zenye Staha (NDWCP III), pamoja na kuimarisha usalama na afya mahali pa kazi kwa kutekeleza mpango wa Vision Zero na mifumo mingine ya ulinzi wa kazi.
Sangu ametaja jambo la tatu kuwa ni kuimarishwa kwa mifumo ya hifadhi ya jamii kupitia Sera ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2023, ambapo zaidi ya wanachama 560,000 wa sekta isiyo rasmi na wanaojiajiri wamefikiwa kupitia usajili wa kidijitali kufikia Machi 2026.
Amesema jambo la nne ni kuanzishwa kwa mfumo wa kielektroniki wa “e-UTATUZI” unaotumiwa na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), ambao umeboresha usimamizi wa migogoro ya kazi kwa kurahisisha wafanyakazi na waajiri kufungua malalamiko na kuwasilisha mashauri mtandaoni kutoka sehemu yoyote nchini.
Jambo la tano ni kuimarishwa kwa mazungumzo ya kijamii ya pande tatu kupitia ushirikiano kati ya Serikali, waajiri na wafanyakazi, hatua iliyowezesha kuwepo kwa kiwango cha chini cha mishahara kwa sekta binafsi kuanzia Januari 1, 2026 pamoja na marekebisho ya sheria za kazi yaliyofanyika mwaka 2025.
Aidha, jambo la sita ni kuendelea kwa ushirikiano kati ya Tanzania na ILO katika kuhakikisha matumizi ya Teknolojia ya Akili Bandia (AI) yanachochea maendeleo endelevu.
Vile vile, Sangu amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na wadau wa kazi wa ndani na wa kimataifa ili kuhakikisha maendeleo ya teknolojia yanatumika kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza tija na kuimarisha ustawi wa wafanyakazi nchini.
Kwa upande wa Wawakilishi wa Waajiri na Wafanyakazi wanaoshiriki Mkutano wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), wameendelea kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi zake za kuimarisha na kudumisha ushirikiano wa wadau wa utatu (Tripartite Partners). Ushirikiano huu umekuwa chachu ya mshikamano na mashauriano ya pamoja katika masuala mbalimbali yanayohusu ajira, haki za wafanyakazi, na ustawi wa waajiri.
Mkutano wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) umetoa fursa kwa washiriki kujadili ajenda muhimu zinazohusu mustakabali wa kazi na maendeleo ya kijamii. Miongoni mwa mada kuu ni manufaa na matumizi ya Teknolojia ya Akili Bandia (AI) katika kukuza ajira zenye staha, kuongeza tija na kuendeleza ukuaji jumuishi wa uchumi. Aidha, pia washiriki wamejadili masuala mengine ya msingi, yakiwemo: utekelezaji wa Mikataba ya ILO; Ushirikishwaji wa Wadau wa Utatu (Tripartism) katika kuimarisha majadiliano; Kazi zenye Staha zitokanazo na majukwaa ya kidigitali; Mageuzi na Usawa wa kijinsia Mahali pa Kazi; kufuatwa kwa Mkataba wa Viwango vya Kazi kwa maeneo yasiyo na Miji Mikuu (Labour Standars (Non-Metropolitan Territories Convention, 1947 (Na. 83) unaolenga kulinda haki za wafanyakazi katika maeneo ya pembezoni.
MWISHO