Mwenyekiti wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala, Prof. Nicolao Joseph Otieno,akionyesha dawa zilizopigwa marufuku kwa waandishi wa habari kuhusu tamko kwa umma kuhusu huduma za Tiba Asili na Tiba Mbadala leo Juni 5,2026 jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala, Prof. Nicolao Joseph Otieno,akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tamko kwa umma kuhusu huduma za Tiba Asili na Tiba Mbadala leo Juni 5,2026 jijini Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini limepiga marufuku matumizi, uingizwaji, usambazaji na uuzaji wa baadhi ya dawa za tiba asili baada ya uchunguzi kubaini uwepo wa kemikali za dawa za kisasa pamoja na viambata hatarishi vinavyoweza kuhatarisha afya za watumiaji.
Akizungumza leo Juni 5,2026 jijini Dodoma na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Baraza hilo,Prof. Nicolao Joseph Otieno, amesema hatua hiyo imechukuliwa kufuatia matokeo ya ufuatiliaji wa dawa za tiba asili uliotekelezwa katika mikoa ya Dodoma, Morogoro, Pwani na Dar es Salaam katika mwaka wa fedha 2025/2026.
Prof. Otieno amesema uchunguzi huo umebaini kuwa dawa ya Powaful Banana Medicine, ambayo baadaye ilibadilishwa jina na kuitwa Banana Medicine, ilikuwa imechanganywa na kemikali za dawa za kisasa za kuongeza nguvu za kiume aina ya Sildenafil na Tadalafil pamoja na dawa za maumivu za Tramadol na Paracetamol bila kuainishwa kwenye lebo wala wakati wa usajili.
Kutokana na ukiukwaji huo, Baraza limefuta rasmi usajili wa dawa hiyo kuanzia Juni 1, 2026 na kumuagiza mtengenezaji wake, Powaful Products Company Ltd, kuiondoa sokoni mara moja.
Aidha, dawa nyingine inayojulikana kwa jina la Vitamax maarufu kama “viasali”, ambayo haikuwa imesajiliwa nchini, imepigwa marufuku kuingizwa, kusambazwa, kuuzwa na kutumika baada ya uchunguzi wa maabara kubaini kuwa ilikuwa na kemikali hizo hizo za dawa za kisasa licha ya kudaiwa kutengenezwa kwa viambata vya mimea tiba.
“Matumizi ya dawa hizi yanaweza kusababisha matatizo makubwa ya kiafya ikiwemo magonjwa ya moyo, figo na ini, shinikizo la damu, utegemezi wa dawa na hata vifo kwa baadhi ya watumiaji,” amesema Prof. Otieno.
Katika hatua nyingine, Baraza limeagiza kuondolewa sokoni kwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy yenye usajili TZ25TM0010 baada ya kubainika kuwa na kiwango kisichokubalika cha sumu kuvu, ambayo inaweza kusababisha saratani ya ini, uharibifu wa figo na kupunguza kinga ya mwili.
Mbali na hatua hizo, Baraza limetoa onyo kali kwa waganga wa tiba asili wanaotoa huduma bila usajili wa kisheria, likikumbusha kuwa kufanya hivyo ni kosa linaloweza kusababisha faini ya shilingi laki tano, kifungo cha miaka miwili au adhabu zote mbili kwa pamoja.
Pia limezitahadharisha taasisi za habari, watangazaji na watumiaji wa mitandao ya kijamii dhidi ya kutangaza dawa au huduma za tiba asili bila kibali rasmi kutoka Baraza. Kwa mujibu wa kanuni zilizopo, wanaokiuka masharti hayo wanaweza kutozwa faini isiyopungua shilingi milioni moja.
Prof. Otieno amesema Baraza limebaini ongezeko la wafanyabiashara wanaotumia virutubisho vya chakula kama dawa za kutibu magonjwa mbalimbali kinyume cha sheria pamoja na kubadili maduka ya virutubisho kuwa kliniki zisizosajiliwa zinazotoa huduma za kitabibu kwa kutumia vifaa visivyotambuliwa kisheria.
Kutokana na hali hiyo, Baraza limetoa maelekezo kwa wazalishaji, wasambazaji na wauzaji wote wa dawa za tiba asili kusajili au kuorodhesha bidhaa zao mara moja. Amesema baada ya miezi sita kuanzia tarehe ya tamko hilo, ukaguzi maalumu utaanza na dawa zote ambazo hazitasajiliwa au kuorodheshwa zitakamatwa na kutaifishwa kwa mujibu wa sheria.
Hata hivyo amewataka wananchi kuhakikisha wanapata huduma za tiba asili kutoka kwa waganga na vituo vilivyosajiliwa pekee, pamoja na kutumia dawa ambazo zimethibitishwa ubora na usalama wake na Baraza.
Prof. Otieno amewakumbusha watoa huduma za tiba asili kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa ya kuambukiza, hususan ugonjwa wa Ebola ambao umeripotiwa katika nchi jirani za Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, kwa kuzingatia kanuni za usafi na kutumia vifaa kinga wanapohudumia wagonjwa.
Baraza limesisitiza kuwa litaendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na taasisi nyingine za Serikali kuhakikisha huduma za tiba asili na tiba mbadala nchini zinakuwa salama, bora na zinazolinda afya za wananchi.