Na Mwandishi Wetu – Gairo, Morogoro
Wakala ya Barabara za vijijini na mijini (TARURA) kupitia mradi wa RISE unaotekelezwa kwa mkopo nafuu toka Benki ya Dunia imekamilisha ujenzi wa barabara ya Iyogwe-Chogohali yenye urefu wa Km 21.5 wilayani Gairo mkoani Morogoro na kuondoa kikwazo cha mawasiliano kati ya kata ya Iyogwe na Chogohali pamoja na wilaya jirani ya Mvomero.
Hayo yamesemwa na Meneja wa TARURA wilaya ya Gairo Mhandisi Simon Masala wakati wa ziara maalum ya kutembelea miradi ya RISE inayotekelezwa chini ya programu ya kuondoa vikwazo barabarani (Bottleneck).
Amesema ujenzi wa barabara hiyo umehusisha ujenzi wa makalavati madogo madogo ya zege tisa na kubwa moja lenye midomo minne ambalo kabla ya ujenzi wake eneo hilo lilikuwa ni kikwazo kikubwa kwa wananchi hao.
“Tulipata fedha kutoka Benki ya Dunia kupitia mradi wa RISE ambapo baada ya kupata fedha hizo tulizielekeza kwenye barabara hii kwa ajili ya kuondoa vikwazo ambavyo wananchi wetu kutoka upande wa Chogohali walikuwa wanashindwa kwenda kupata huduma katika wilaya yetu ya Gairo”.
Amesema vijiji vya ng’ambo ya pili ya mto vinategemea huduma zote za kijamii kama vile vituo vya afya na shule ya sekondari upande wa Iyogwe na makao makuu ya wilaya mjini Gairo kwa hiyo walikuwa wanapata shida hasa kipindi cha masika kwani walikuwa wanashindwa kuvuka hivyo kulazimika kusubiri mpaka maji yapungue.
Kwa upande wa kiuchumi, Mhandisi Masala amesema barabara hiyo inaunganisha wilaya ya Gairo na wilaya jirani ya Mvomero na kuongeza kuwa kabla ya ujenzi huo wananchi kutoka pande zote walikuwa hawawezi kuingia kwenye wilaya hizo kupitia barabara hiyo ambayo ni fupi na kulazimika kuzunguka kupitia njia nyingine ambayo ina urefu wa zaidi ya Km 60.
“Baada ya kuifungua barabara hii wilaya jirani ya Mvomero na kata zao za jirani wanakuja kupata huduma hapa wilaya ya Gairo kwa hiyo wananchi wanapata huduma kwa urahisi zaidi katika muunganiko wa kiuchumi kwa kuuza na kununua mazao yao na bidhaa nyingine”, amefafanua.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Iyogwe Bw. Richard Yeremia Kagoda ameishukuru serikali kwa mradi huo kwani kabla ya ujenzi walikuwa wanapata changamoto mbalimbali hasa katika masuala ya kiuchumi, kiutawala, kiusalama na hata shughuli za kijamii.
Naye, Bi. Anna Allan Mkamilo mkazi wa kijiji cha Iyogwe ametoa ushuhuda wake kuwa kabla ya ujenzi wa barabara na daraja walikuwa wakipoteza watu wao muhimu hususani wajawazito ambao walikuwa wakitoka maeneo ya mashambani na wengine kijiji jirani cha Masimbani ambao kipindi cha masika walishindwa kuvuka na kupelekea wengine kujifungulia sehemu ambayo sio salama.
