Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 11,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeendelea kufanya mapinduzi makubwa katika sekta ya afya baada ya kuimarisha huduma za matibabu ya ubingwa na ubingwa bobezi nchini, hatua iliyowezesha wananchi wengi kupata matibabu ya kisasa ndani ya Tanzania badala ya kusafiri nje ya nchi kama ilivyokuwa awali.
Hayo yameelezwa leo bungeni na Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, wakati akiwasilisha mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka wa fedha 2026-2027,amesema Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2021/2022 hadi Machi 2026, hospitali za rufaa na taasisi maalum za afya zimefanikiwa kutoa huduma mbalimbali za kibingwa zilizogusa maisha ya maelfu ya wananchi.
Mhe.Mchengerwa amesema kuwa wagonjwa 170 wamefanyiwa upandikizaji wa figo huku wagonjwa 57 wakipatiwa huduma ya upandikizaji wa uloto. Aidha, wagonjwa 102 walipatiwa vifaa vya usikivu na wengine 200 kufanyiwa uwekaji wa puto tumboni.
Huduma nyingine zilizotolewa ni pamoja na kuondoa mawe kwenye mfumo wa mkojo kwa kutumia mawimbi mshtuko kwa wagonjwa 510, upandikizaji wa nyonga na magoti kwa wagonjwa 1,791 pamoja na upasuaji wa mgongo kwa wagonjwa 1,688.
“Katika hatua inayoonyesha kukua kwa teknolojia ya tiba nchini, wagonjwa 98 walifanyiwa upasuaji wa kibiongo huku wagonjwa 2,095 wakifanyiwa upasuaji wa vichwa vikubwa na mgongo wazi. Pia wagonjwa 1,246 walifanyiwa upasuaji wa magoti kwa njia ya matundu.”amesema
Serikali imefanikiwa kutoa huduma za hali ya juu katika tiba za moyo, ubongo na saratani. Wagonjwa 1,208 walifanyiwa upasuaji wa ubongo kwa kufungua kichwa na wengine 785 kufanyiwa upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu.
Katika huduma za moyo, wagonjwa 73 walifanyiwa upasuaji wa moyo kwa kufungua kifua huku wagonjwa 2,074 wakifanyiwa huduma ya kuzibua mishipa ya moyo. Aidha, wagonjwa 34 walifanyiwa upandikizaji wa vifaa vya kurekebisha mapigo ya moyo.
Kwa upande wa matibabu ya saratani, wagonjwa 6,097 walifanyiwa upasuaji wa magonjwa ya saratani huku wagonjwa 4,024 wakipatiwa tiba ya immunotherapy. Vilevile, wagonjwa 10,056 walipata tiba ya mionzi ya ndani na wagonjwa 731 kufanyiwa uchunguzi kwa kutumia teknolojia ya PET-CT Scan.
Serikali imesema uwekezaji huo mkubwa umechangia kupunguza gharama kwa wananchi waliokuwa wakisafiri nje ya nchi kutafuta huduma hizo huku pia ukiifanya Tanzania kuwa kitovu cha tiba kwa nchi jirani.
Kutokana na ubora wa huduma hizo, wagonjwa 26,770 kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika yakiwemo Comoros, Democratic Republic of the Congo, Zambia, Malawi, Kenya, Rwanda na Uganda wamekuja nchini kupata huduma za matibabu.