Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 11,2026 bungeni Dodoma.

Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa,akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Mei 11,2026 bungeni Dodoma.
Na.Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeendelea kuandika historia mpya katika sekta ya afya baada ya kufanikisha kupungua kwa kiasi kikubwa kwa vifo vitokanavyo na uzazi nchini, hatua inayotajwa kuwa matokeo ya uwekezaji mkubwa katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto.
Hayo yameelezwa leo bungeni na Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, wakati akiwasilisha mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka wa fedha 2026-2027,ambapo ameeleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita zaidi ya Shilingi Trilioni 1.2 zimeelekezwa katika miradi ya afya kupitia diplomasia ya afya, jambo lililowezesha kuboreshwa kwa huduma muhimu kwa mama na mtoto nchini kote.
Amesema kuwa idadi ya wodi maalum za watoto wachanga imeongezeka kutoka 49 mwaka 2021/2022 hadi kufikia 438 mwezi Machi 2026. Aidha, vituo vya uchunguzi wa awali wa saratani ya mlango wa kizazi katika ngazi ya msingi vimeongezeka kutoka 732 hadi 1,700 katika kipindi hicho.
Serikali pia imeimarisha huduma kupitia mpango wa Madaktari wa Dkt. Samia ambapo watumishi wa afya 29,129 wamepatiwa mafunzo kazini huku wananchi 286,381 wakihudumiwa kupitia mpango huo.
Katika hatua nyingine, upatikanaji wa dawa muhimu za afya ya uzazi, mama na mtoto umefikia asilimia 85. Dawa hizo ni pamoja na oxytocin na misoprostol za kuzuia damu kuvuja kwa wingi wakati wa kujifungua, magnesium sulfate ya kutibu kifafa cha mimba pamoja na dawa za watoto za ORS/Zinc na amoxycilline.
Mafanikio hayo yamechangia kushuka kwa kiwango cha vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022.
Kutokana na mafanikio hayo makubwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ametambuliwa barani Afrika kama kinara wa huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto.
Serikali imesema itaendelea kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo kwa lengo la kupunguza zaidi vifo vya uzazi kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2030, hatua itakayowezesha Tanzania kuvuka malengo ya dunia ya kupunguza vifo vya uzazi hadi chini ya vifo 70 kwa kila vizazi hai 100,000.
“Nichukue fursa hii kuwafahamisha waheshimiwa wabunge na wananchi kuwa, Mheshimiwa Rais ameendelea kutambuliwa kama Rais wa mfano aliyefanya vizuri katika kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vitokanavyo na uzazi kwa kipindi kifupi tangu kuingia madarakani,”amesema Waziri Mchengerwa
Serikali imeeleza kuwa dhamira ya dhati ya Rais katika kuboresha huduma za afya imekuwa chachu ya mafanikio hayo, huku lengo kuu likiwa kuhakikisha hakuna mwanamke anayepoteza maisha wakati wa kujifungua.