Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema matukio ya vurugu yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 yalikuwa ya kushtua na kutikisa ustawi wa taifa, akibainisha kuwa uchunguzi rasmi umebaini kuwa yalipangwa kwa makusudi, yaliratibiwa na pia kufadhiliwa ili kuvuruga mchakato mzima wa uchaguzi na kudhoofisha amani ya nchi.
Rais Samia ameyasema hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam wakati alipokabidhiwa rasmi ripoti ya Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea katika kipindi cha uchaguzi huo.
Amesema ni muhimu kwa Watanzania kukubali na kuzungumza ukweli kuhusu kilichotokea, akisisitiza kuwa matukio hayo ni funzo kubwa linalopaswa kutumika kuimarisha mustakabali wa taifa na kulinda amani ya kudumu.
“Tusijidanganye, yaliyotokea wakati ule yalitikisa taifa letu. Kwa kweli yalikuwa changamoto kubwa na tumepata somo muhimu,” alisema Rais Samia.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya tume, imebainika kuwa baadhi ya watu waliohusika katika vurugu hizo walikuwa wamepata mafunzo maalum, na walitumia vifaa vya uhalifu vilivyolenga kuharibu miundombinu muhimu ya nchi pamoja na kusababisha hofu na taharuki kwa wananchi.
Aidha, ripoti hiyo inaeleza kuwa lengo kuu la matukio hayo lilikuwa kuvuruga mchakato wa uchaguzi, kushambulia miundombinu ya msingi ya taifa, pamoja na kuathiri utoaji wa huduma za kijamii ili hatimaye kudhoofisha uchumi na utendaji wa Serikali.
“Vurugu zilianza siku ya uchaguzi, zikilenga mfumo mzima wa nchi,” aliongeza Rais Samia.
Katika hotuba yake, Rais Samia pia amevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa jitihada zao za haraka na za ufanisi zilizosaidia kurejesha hali ya utulivu wakati wa na baada ya matukio hayo, hatua iliyosaidia kuzuia madhara makubwa zaidi kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria ili kuhakikisha kuwa amani, utulivu na demokrasia ya nchi vinalindwa kwa nguvu zote.


