Arusha
Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara zinazoingia katika uwanja utakaotumika kwa mashindano ya AFCON jijini Arusha.
Mhandisi Seff amesema kwamba ziara hiyo imelenga kujionea hatua za utekelezaji wa mradi wa barabara zenye urefu wa kilomita 21.4 ambapo kazi tayari zimeanza katika sehemu ya barabara ya Essuri.
Amesema serikali imejipanga kuhakikisha miundombinu hiyo inakamilika kwa wakati na kuongeza kuwa maeneo ambayo bado hayajaanza yanasubiri kukamilisha taratibu za fidia kwa wananchi watakaoathiriwa na mradi huo huku mkakati ukiwa ni kuendelea kuzungumza nao ili kutoa ushirikiano na kuruhusu kazi ziendelee bila vikwazo.
“Lengo la Serikali ni kuhakikisha barabara hizi zinakamilika ifikapo Mei mwaka 2027 ili ziwe tayari kabla ya mashindano ya AFCON,” amesema Mhandisi Seff.
Aidha, amesema mradi huo unatekelezwa kwa utaratibu wa Sanifu na Jenga (Design and Build) unaotumika pale ambapo muda ni mchache huku hatua zote za ununuzi tayari zikikamilika.
Ameeleza kuwa TARURA itaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mkandarasi anakamilisha kazi kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa sanjari na ratiba ya mashindano hayo makubwa ya Mataifa ya Afrika.
Ameongeza kuwa kwa sasa Mkandarasi M/s China Railway Construction Engineering Group tayari ameanza kazi ambapo ameanza na barabara ya Essuri yenye urefu wa kilomita 2.45 pia kutajengwa daraja lenye urefu wa mita 100.
Kwa upande wa barabara ya Lendita yenye kilomita 2.75, Mhandisi Seff amesema barabara hiyo itajengwa pamoja na daraja katika awamu ya pili ya mradi huku barabara hiyo ikitarajiwa kuwa ya njia nne.
Ameongeza kusema pia barabara ya Mateves yenye kilomita 6.5 itajengwa kwa sehemu mbili ambapo kilomita 5.5 zitakuwa njia mbili na kilomita 1 itakuwa njia nne.
Mtendaji Mkuu huyo amesema kukamilika kwa mradi huo kutaleta mafanikio makubwa kwa Taasisi hiyo kwa kupata uzoefu wa kusimamia miradi ya Sanifu na Jenga, huku wananchi wakinufaika kwa kuondokana na changamoto ya miundombinu katika maeneo hayo.
Vilevile, amesema wakazi wa maeneo yanayozunguka mradi huo watapewa kipaumbele cha ajira na amewataka vijana kujitokeza kupata ajira na kutumia fursa hiyo kujiongezea kipato pamoja na uzoefu wa kazi.
Kwa upande mwingine amewataka wasimamizi wa mradi huo kusimamia kwa karibu utekelezaji wake kwani mashindano hayo yanatarajiwa kuanza Julai mwakani.
Naye, Mhandisi Mshauri kutoka kampuni ya M/s Afrisa Construction Engineering Group Bw. Idephonce Karol amesema mradi huo ulianza rasmi tarehe 1 Aprili, 2026 na kwa sasa hatua za awali zinaendelea vizuri.
Amesema tayari wamehamasisha timu ya wataalamu, kufanya upimaji wa maeneo yote matatu ya barabara, uchunguzi wa udongo, tathmini ya vifaa vya ujenzi pamoja na kusafisha sehemu ya barabara ya Essuri urefu wa kilomita 1.8.
“Tumejipanga kikamilifu na tunafahamu umuhimu wa mradi huu hivyo tutafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati,” amesema Karol.
