Featured Kitaifa

SIKU 100 ZA RAIS SAMIA:WIZARA YA UCHUKUZI YAZINDUA MAANDALIZI YA UPANUZI WA BANDARI, MAPATO YAONGEZEKA KWA ZAIDI YA SH. TRILIONI 1.4

Written by Alex Sonna

WAZIRI  wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Februari 1,2026 katika Mji wa Kiserikali Mtumba jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan katika siku 100 za kipindi cha Uongozi wake katika awamu ya sita.

WAZIRI  wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawaakisisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Februari 1,2026 katika Mji wa Kiserikali Mtumba jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan katika siku 100 za kipindi cha Uongozi wake katika awamu ya sita.

Na.Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeanza maandalizi ya upanuzi mkubwa wa Bandari ya Dar es Salaam pamoja na ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuimarisha sekta ya usafirishaji na lojistiki nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari  leo Februari 1,2026 kuhusu utekelezaji wa ahadi za Rais  Dkt.Samia Suluhu Hassan,Prof. Mbarawa amesema  hatua hiyo pia inaambatana na utekelezaji wa miradi mingine muhimu ikiwemo Kurasini Logistics Terminal, Bandari ya Kemondo – Bukoba, Bandari ya Mbamba Bay na Bandari ya Kisiwa Mgao mkoani Mtwara.

 “Maboresho hayo yameanza kuleta matokeo chanya kiuchumi, ambapo mapato ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) pamoja na wawekezaji binafsi yameongezeka kwa zaidi ya Shilingi bilioni 290, huku makusanyo ya forodha yakiongezeka kwa zaidi ya Shilingi trilioni 1.17 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita.”amesema Prof. Mbarawa

Aidha Prof. Mbarawa amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa Kituo cha Utafutaji na Uokoaji (MRCC) katika Ziwa Victoria, kununua boti ya wagonjwa (Ambulance Boat), pamoja na boti nne za uokoaji kwa ajili ya maziwa makuu na ukanda wa Bahari ya Hindi.

Amesisitiza kuwa hatua hizo zinalenga kulinda maisha ya wananchi na mali zao, sambamba na kuimarisha uwezo wa nchi katika kukabiliana na ajali za majini.

Kwa upande wa usafiri wa anga, Waziri huyo amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa Jengo la Viongozi katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), pamoja na kuanza maandalizi ya ujenzi wa viwanja vipya vya ndege Serengeti na Kagera.

Aidha, amesema Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) imeendelea kupanua wigo wa huduma zake na sasa inahudumia jumla ya vituo 32 ndani na nje ya Bara la Afrika.

 “Maboresho ya miundombinu ya usafirishaji yameifanya Tanzania kuendelea kuwa lango kuu la biashara kwa nchi zisizo na bandari ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Zambia, Rwanda, Burundi, Uganda na Malawi.”amesema 

Ameongeza kuwa juhudi hizo zinaijenga Tanzania kuwa kitovu muhimu cha lojistiki katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Amesema kuwa katika kipindi hicho kifupi, Serikali imefanikiwa kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta ya reli, bandari, usafiri wa majini, anga pamoja na kuimarisha usalama wa usafiri majini na uunganishwaji wa kikanda na kimataifa.

 “Serikali imekamilisha hatua muhimu za ufufuaji wa Reli ya TAZARA, ikiwemo kusaini mkataba wa uboreshaji na Kampuni ya CCECC ya China kwa ushirikiano wa Serikali za Tanzania na Zambia. Mradi huo ulizinduliwa Novemba 2025 na unatarajiwa kuanza utekelezaji Juni 2026, hatua itakayoongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam na kuimarisha biashara na nchi za Kusini mwa Afrika.”amesema Prof.Mbarawa

Aidha, Shirika la Reli Tanzania (TRC) limeanza kujitegemea kifedha bila ruzuku ya mshahara, limeanzisha Kampuni Tanzu ya TANRAIL kwa ajili ya kukuza mapato, na kuendelea kuendesha reli za SGR na MGR ambazo zimesafirisha zaidi ya abiria 838,000 na tani zaidi ya 85,000 za mizigo ndani ya siku 100.

Hata hivyo ametoa wito kwa watanzania na wadau wote kushirikiana na Serikali katika kulinda na kutunza miundombinu hiyo ili iwe na manufaa endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho. 

Mafanikio yaliyopatikana ndani ya siku 100 ni mwanzo tu wa safari ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuijenga Tanzania yenye miundombinu ya kisasa, salama na yenye tija.

About the author

Alex Sonna