Featured Kitaifa

SERIKALI YAJIPANGA KUIMARISHA USAWA WA KIJINSIA KUPITIA SERA NA MIPANGO JUMUISHI

Written by Alex Sonna

 Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Jinsia, Badru Abdunuru,akizungumza  wakati akifunga mafunzo ya Ujumuishaji wa bajeti kwa maafisa wa Serikali kutoka Wizara mbalimbali kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu,leo Septemba 3,2025 jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

KATIBU  Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo, taasisi na sekta binafsi kuhakikisha masuala ya usawa wa kijinsia yanapewa kipaumbele katika sera, mipango na bajeti.

Hayo yamesemwa leo Septemba 3, 2025 Jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Jinsia, Badru Abdunuru kwa niaba ya  Dkt. John Jingu, wakati akifunga mafunzo ya Ujumuishaji wa bajeti kwa maafisa wa Serikali kutoka Wizara mbalimbali.

Bw.Badru amesema kuwa  ushirikiano huo umekuwa chachu ya mafanikio katika sekta mbalimbali.

Amesema kupitia ushirikiano kati ya Serikali na Umoja wa Ulaya, hususan kupitia programu ya Gender Transformative Action, Breaking the Glass Ceiling (GTAP), kumekuwepo na mafanikio makubwa katika utekelezaji wa ajenda ya kijinsia katika sekta za elimu, afya, maendeleo ya jamii na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.
“Dhamira ya Serikali ni kuimarisha usawa wa kijinsia na kuhakikisha kila Mtanzania ananufaika na fursa zilizopo, anashiriki kikamilifu na anakua huru dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia,” alisema Dkt. Jingu akirejea Dira ya Taifa ya 2050 iliyozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Julai 17, 2025.
“Dhamira ya Serikali ni kuimarisha usawa wa kijinsia na kuhakikisha kila Mtanzania ananufaika na fursa zilizopo, anashiriki kikamilifu na anakua huru dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia,” amesema Bw.Badru akirejea Dira ya Taifa ya 2050 iliyozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Julai 17, 2025.
Aidha, ameeleza  kuwa wizara yake imeandaa mazingira wezeshi ya utekelezaji kupitia Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia (2023), Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA II 2024/25–2028/29), Jukwaa la Kizazi chenye Usawa, Ajenda ya Kitaifa ya Afya na Maendeleo ya Vijana Balehe, Mpango wa Kitaifa wa Wanawake, Amani na Usalama, pamoja na Kampeni ya Inspire to Lead (2025–2029).

Kwa upande wake  Mwalilishi kutoka Umoja wa Ulaya (EU) Alexandra Pissat amesema ili kuleta usawa wa kijinsia ni muhimu kuzingatia bajeti katika masuala ya jinsia, kufanya tathmini na ufuatiliaji ili kuendelea kuondoka changamoto mbalimbali ambazo zinaweza kurudisha nyumba mipango ya kuleta usawa wa kijinsia nchini.

“Mabadiliko chanya na maendeleo kwa jamii yanapatikana tu ikiwa usawa wa kijinsia unazingatiwa katika mipango ya Serikali katika utekelelezaji wa ajenda mbalimbali za kuwawezesha wanawake katika masuala ya jinsia.” amesisitiza Alexandra

Naye  Mwakilishi kutoka Wizara ya Maji, Susan Magoli amesema mafunzo hayo yamekuwa msaada mkubwa kwani yanaelekeza kutoa kipaumbele katika kutenga bajeti kwa kuhusisha masuala ya usawa wa kijinsia jambo ambalo litachangia maendeleo na ushiriki wa wanawake katika uwezeshaji na uongozi.

Mafunzo hayo yalishirikisha washiriki zaidi ya 200 kutoka Wizara na Wakala za Serikali yakiandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU), yakilenga kutoa elimu ya ujumuishaji wa masuala ya jinsia katika bajeti ili kuleta usawa wa kijinsia, kuongeza uelewa na kuwapa washiriki zana, maarifa na ujuzi unaohitajika ili kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake katika mipango na bajeti za Wizara za kisekta, kwa kuzingatia Sera ya Jinsia 2023 na Dira ya 2050.

About the author

Alex Sonna