Featured Kitaifa

RAIS SAMIA ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUFUATIA AJALI YA GARI MKOANI MBEYA

Written by mzalendoeditor

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 

SALAMU ZA RAMBIRAMBI 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtumia  salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera kufuatia  ajali ya gari iliyotokea tarehe 07 Juni, 2025 majira ya saa 01 usiku katika eneo la Mlima  Iwambi, Tarafa ya Utengule Usongwe, Wilaya ya Mbalizi, barabara kuu ya Mbeya– 

Tunduma. 

Ajali hiyo ilihusisha lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 830 EDP/T 148 CTD  lililokuwa limebeba shehena ya unga kutoka Dar es Salaam kuelekea Zambia, lililogonga  kwa nyuma magari mawili namba T 257 DVP aina ya Mitsubishi Rosa na T 185 DMF aina  ya Toyota Lite Ace na hatimaye kuanguka katika bonde la Mto Mbalizi. 

Chanzo cha ajali kinasadikiwa kuwa ni uzembe wa dereva wa lori kushindwa kulimudu  gari kwenye mteremko. 

Katika ajali hiyo, watu 28 wamepoteza maisha wakiwemo wanawake 12 (kati yao watoto  wawili) na wanaume 16 (kati yao watoto wawili). Hadi sasa, miili 19 imetambuliwa na tisa haijatambuliwa. Aidha, watu nane (wanaume sita na wanawake wawili) wamejeruhiwa.  

Rais Dkt. Samia anatoa wito kwa madereva wote nchini kuzingatia sheria za usalama  barabarani. 

Vilevile, Rais Dkt. Samia anawapa pole wafiwa wote na anaungana na familia za marehemu  na wote walioguswa na msiba huu mkubwa katika kipindi hiki kigumu cha majonzi. 

Mwenyezi Mungu awape majeruhi nafuu ya haraka na azilaze roho za marehemu mahali  pema peponi. Amin. 

Shaaban Kissu 

Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu

About the author

mzalendoeditor