Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Serikali imethibitisha kuwa inaendelea na hatua za awali kuelekea ujenzi wa daraja la kudumu linalounganisha Kijiji cha Negero katika Wilaya ya Kilindi, mkoani Tanga, ili kuboresha miundombinu na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo.
Akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Kilindi, Mhe. Omar Mohamed Kigua, Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mhe. Zainab Katimba, amesema serikali tayari imeshakamilisha usanifu wa daraja hilo, ambao uligharimu shilingi milioni 70 na kukamilika mwezi Machi 2025.
“Serikali inatambua umuhimu wa daraja hili kwa maendeleo ya wananchi wa Kijiji cha Negero. Hivi sasa tupo kwenye hatua ya kupitia taarifa ya usanifu ili kupata gharama halisi za ujenzi. Baada ya hatua hiyo kukamilika, daraja litaombewa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wake,” alisema Mhe. Katimba wakati akihutubia Bunge Jijini Dodoma.
Kwa sasa, wananchi wa eneo hilo wanategemea kivuko cha chuma kwa waenda kwa miguu (Pedestrian Suspension Bridge) chenye urefu wa mita 100, kilichojengwa na kukamilika mwezi Desemba 2021 kwa gharama ya shilingi milioni 66.68, ili kuwasaidia kuvuka Mto Negero kwa urahisi.
Mhe. Katimba aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara na madaraja hususan katika maeneo ya vijijini ili kurahisisha usafiri na kuongeza fursa za kiuchumi kwa wananchi.