Featured Michezo

PROF.KABUDI ATAJA MAFANIKIO LUKUKI YA WIZARA YAKE MIAKA MINNE YA RAIS SAMIA

Written by mzalendoeditor

WAZIRI  wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi, akizungumza na Waandishi wa Habari leo Aprili 14,2025 jijini Dodoma kuhusu Mafanikio ya Wizara hiyo katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan.

…….

WAZIRI  wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Profesa Palamagamba Kabudi amesema katika kuboresha sekta ya michezo nchini, Serikali imetoa shilingi bilioni 161.9 ili kukarabati na kujenga miundombinu ya michezo nchini, ikiwa pia ni sehemu ya maandalizi ya michuano ya AFCON 2027.

Prof. Palamagamba Kabudi,ameyasema hayo leo Aprili 14,2025 jijini Dodoma wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Mafanikio ya Wizara hiyo katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan.

Waziri Kabudi ameeleza kuwa miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa viwanja vya mpira wa miguu Arusha na Dodoma vyenye uwezo wa kutumiwa na watazamaji elfu 32 kila kimoja kwa mara moja, ukarabati wa Uwanja wa Uhuru na Uwanja wa Benjamin Mkapa mkoani Dar es Salaam, ujenzi wa vituo vya mazoezi na kupumzika wananchi kwa Dar es Salaam na Zanzibar, ujenzi viwanja, hosteli na akademia ya michezo katika Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya kilichopo mkoani Mwanza.

“Sekta ya michezo nchini inakuwa kwa kasi ambapo Tanzania ni kati ya nchi tatu za Afrika zilizofuzu katika mashindano saba tofauti yanayoendeshwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF).”amesema Prof.Kabudi

Amesema kuwa ili  kuhakikisha shughuli za Michezo zinafanyika kwa ufanisi Serikali ya Awamu ya Sita , katika kipindi chake cha miaka Minne imeanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Michezo ambapo jumla ya shilingi bilioni 10.657 zimetolewa.

“Mafanikio mengine yaliyopatikana kupitia fedha hizo ni kujenga na kukarabati miundombinu ya michezo, kuwezesha mafunzo kwa wataalamu mbalimbali wa michezo na kuwezesha Vyama na Mashirikisho ya michezo nchini,”amesema Prof.Kabudi

Hata hivyo ameongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imefanikiwa kuhuisha na kuendeleza wazo la muda mrefu la ujenzi wa Sports and Arts Arena mradi huo wa kisasa, unaotarajiwa kugharimu takribani Shilingi bilioni 300 ambapo unatarajiwa kufadhiliwa kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka nchini Korea.

“Na utakapokamilika utakuwa ni moja ya vituo vikubwa vya michezo na sanaa katika Ukanda wa Afrika Mashariki, ukiwa kichocheo cha ajira, burudani, utalii na maendeleo ya vipaji vya vijana,”ameongeza.

Kuhusu Mechi ya Watani Simba na Yanga,Serikali imesema kuwa imepanga kuzungumza na wadhamini wa dabi hiyo ya kariakoo na kuwataka Watanzania na mashabiki wa dabi hiyo kuwa na subira wakati mazungumzo hayo yakiendelea.

Dabi ya Kariakoo ilipangwa kuchezwa Machi 8, 2025 lakini haikuchezwa kutokana na timu ya Simba kushindwa kuleta timu uwanjani hivyo serikali ilianza mazungumzo na timu zote mbili kuhusu mustakabali wa mechi hiyo.
“Mazungumzo kuhusu dabi hiyo yamefikia hatua nzuri baada ya mazungumzo yaliyofanyika kwa klabu za Simba na Yanga.”amesema
Amesema kwa mujibu wa kanuni za CAF serikali hairuhusiwi kuingilia masuala ya mpira ila kinachoendelea ni kuzikutanisha timu hizo ili waweze kujua muafaka kuhusu dabi hiyo ya Kariakoo.
“Ni kweli Machi 27 tulikutana na timu za Simba na Yanga na nina mpango sasa wa kukutana na wadhamini wa Kariakoo Derby benki ya NBC lengo letu lilikuwa ni kuwakutanisha wao wakutane waongee. Masuala ya ligi yanasimamiwa na TFF na bodi ya ligi na Waziri hawezi kuyaingilia kwa kanuni za FIFA kama mnavyofahamu,”
Amesema dabi ya Kariakoo imepata umaarufu wa Kimataifa na sasa ina wafuasi wengi kwa hiyo wizara ilichofanya ilikuwa ni kuwaleta pamoja ili waanze mchakato wa wao kufikia maridhiano na maelewano ambayo hatimaye yatafika mahali ambapo wale wenye dhamana ya kisheria na kikanuni kutoa tamko watatoa tamko.
Profesa Kabudi amesema uwanja wa Mkapa umefanyiwa matengenezo makubwa kwa ajili ya mashindano ya CHAN na yale ya AFCON ambayo yanatarajiwa kufanyika uwanjani hapo.
Amesema baada ya mechi ya Kimataifa kati ya Simba na Al Masry serikali ilitangaza kuufunga uwanja huo kwa ajili kuukarabati kwa ajili ya michuano ya CHAN na AFCON
Amesema uwanja huo kwa sasa umeshafanyiwa ukarabati mkubwa kwani ulikuwa haujawahi kufanyiwa ukarabati tangu ulipoanza kutumika ambapo mpaka sasa viti vipya 40,000 vimeshawekwa, bado viuti 20,000, wameshafunga taa 360 uwanjani hapo, wameshafunga CCTV kamera na kukarabati vyoo vya uwanjani hapo.
“Kuna matengenezo makubwa yamefanyika kwani kabla ya mechi ya simba na Al Masry mvua kubwa ilinyesha kwa muda wa saa mbili na baada ya nusu saa timu zikaingia uwanjani kwa hiyo tulilazimika kuufunga uwanja huo ili ufanyiwe ukarabati,” amesema Profesa Kabudi
Kufuatia Rais wa Klabu ya Yanga na Mwenyekiti wa Umoja wa Vilabu Afrika (ACA), Hersi Said kupata tuzo kutoka World Football Summit (WFS), ya kuthamini mchango wake wa kuunganisha vilabu vya soka Afrika, Waziri Profesa Kabudi amesema kuwa atamwandikia barua ya pongezi kwa kupata tuzo hiyo.

Katika hatua nyingine   Prof.  Kabudi amesema kupitia R4 za Rais Samia zimesababisha kuongezeka kwa uhuru wa vyombo vya habari na kuiwezesha Tanzania kupanda kwenye viwango vya uhuru wa vyombo vya habari duniani kutoka nafasi ya 143 mwaka 2023 hadi nafasi ya 97 mwaka 2024 na imani yao itaendelea kupanda zaidi.

Prof. Kabudi amesema kuwa,Wizara hiyo imefanikiwa kuleta utulivu ndani ya sekta ya habari, ambapo Vyombo vya Habari vilivyokuwa vimefungiwa kwa makosa mbalimbali vilifunguliwa.

“Hii inaonesha jitihada za dhati za Rais Samia za kuimarisha sekta ya habari nchini, mpaka kufikia mwezi Machi mwaka huu, Tanznia ilikuwa na vyombo vya habari 1042 vilivyosajiliwa ambapo kati ya hivyo, Magazeti ni 372, Vituo vya Redio 247, Vyombo vya Habari Mtandao 355 na Vituo vya Televisheni 68,”amesema.

Prof. Kabudi ameongeza kuwa katika kuonesha utawala wa mfano kwa vitendo, ikiwemo kusimamia kwa mafanikio makubwa utekelezaji wa sheria na miongozo inayolenga kuboresha tasnia ya habari nchini, Serikali ya awamu ya sita, katika kipindi cha miaka minne, imefanikisha kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati ya waandishi wa habari kama inavyoelekezwa na Sheria ya Huduma za Habari Sura ya 229.

“Bodi hii, ambayo ni ya kwanza kuanzishwa tangu kupitishwa kwa sheria hiyo, ilizinduliwa rasmi tarehe 3 Machi, 2025, hili ni fanikio kubwa na la kihistoria katika kulinda na kukuza uhuru, ubora na uwajibikaji katika sekta ya habari nchini Tanzania,”ameongeza.

About the author

mzalendoeditor