Featured Kitaifa

TEA YAUNGA MKONO SERA MPYA YA ELIMU KUBORESHA  MIUNDOMBINU NA VIFAA VYA AMALI SHULE 20 NCHINI

Written by mzalendoeditor
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha akizungumza na waandishi wa Habari katika maonesho ya Uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023 yanayofanyika leo 1,2025 jijini Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA
KATIKA kutekeleza Sera mpya ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la Mwaka 2023, Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imetenga shilingi bilioni 3 kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu na vifaa mbalimbali vya mafunzo ya amali kwa shule 20 nchini.
Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha, ameyasema hayo katika banda la TEA alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa hafla ya uzinduzi wa sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la mwaka 2023 iliyozunduliwa na Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Dkt.Kipesha amesema kuwa wajibu wao ni kuhakikisha wanaunga mkono utekelezaji wa Sera hiyo ya Elimu kwa kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia kwa maana ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, maabara za Sayansi, nyumba za walimuna vifaa mbalimbali vya mafunzo ya amali kama michezo, ushoni, mapishi, kilimo, sanaa na TEHAMA
Aidha amesema kuwa watahakikisha wanaimarisha miundombinu ya elimu kote nchini kuunga mkono utekelezaji wa sera ya elimu kwa kuwa na miundombinu na vifaa vya mafunzo ya amali.
“Jukumu letu kubwa ni kuimarisha na kuboresha miundombinu ya kujifunzia na kufundishia kwa kujenga vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo, nyumba za walimu, maabara, mabweni pamoja na kuweka vifaa mbalimbali vya elimu vya mafunzo ya amali.
“Kwa sasa tumetenga shilingi bilioni 3 kwa ajili ya miundombinu ya amali kwenye shule 20 hapa nchini pamoja na vifaa mbalimbali vya amali ambavyo vitakuwa mkombozi na kuchochea kukua kwa elimu bora na ya kiwango”amesema Dkt.Kipesha
Akizungumzia sera mpya ya elimu Dkt.Kipesha,amesema kuwa elimu ya Tanzania sasa inaenda kuwa elimu ya kimataifa zaidi na itakayowapeleka vijana wengi katika soko kwani vijana wengi watakuwa na elimu pamoja na ujuzi.
Hata hivyo ameeleza kuwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuwakomboa vijana wa Kitanzania kwa kuboresha sera ya elimu na mafunzo ambapo vijana wengi wataweza kujiajiri au kuajiriwa mahali popote nchini kulingana na ujuzi watakaoupata mashuleni.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha akizungumza na waandishi wa Habari katika maonesho ya Uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023 yanayofanyika leo 1,2025 jijini Dodoma.

Wadau mbalimbali wakitembelea banda la TEA katika maonesho ya Uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023 yanayofanyika leo 1,2025 jijini Dodoma.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Dkt. Erasmus Kipesha ,akiwa katika picha ya pamoja katika Banda la TEA katika maonesho ya Uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023 yanayofanyika jijini Dodoma leo tarehe 01 Februari 2025.

About the author

mzalendoeditor