Featured Kitaifa

RC TANGA ATOA NENO KWA WANUNUZI WA ZAO LA MWANI

Written by mzalendo

 

Mkuu wa Mkoa wa Tanga akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea wakulima wa zao hilo katika Mtaa wa Sahare Kijijini Kata ya Mzingani Jijini Tanga ambao pia alizungumza na wakulima wa zao hilo kwenye wilaya za Tanga,Mkinga ,Muheza na Pangani ikiwa ni kuelekea Shamrashamra za kuelekea miaka 60 ya Muungano.

 

MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian akitoka kukagua zao la Mwani wakati wa ziara yake 

 

 

Na Oscar Assenga, TANGA.

MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian amewataka wanunuzi wa zao la mwani mkoani humo kuheshimu mikataba wanayoingia na wakulima ili waweze kulima kwa tija na hivyo kuweza kujikwamua kimaendeleo.

Amesema kutokuheshimu mikataba hiyo hawatakubali kuona linatokea badala yake wataona namna ya kufatuta njia nyengine za kuwahudumia ikiwemo mabenki kwa ajili ya kuwawezesha kupata mikopo yenye riba ndogo na nafuu.

RC Batilda aliyasema hayo  wakati wa ziara ya kutembelea wakulima wa zao hilo katika Mtaa wa Sahare Kijijini Kata ya Mzingani Jijini Tanga ambao wametokea kwenye wilaya za Tanga,Mkinga ,Muheza na Pangani ikiwa ni kuelekea Shamrashamra za kuelekea miaka 60 ya Muungano.

Ambapo pia alitembelea shamba la wakulima wa Mwani pamoja na kugawa kofia,mabuti ,nyundo,kamba na taitai ili kuweza kuwawezesha wakulima hao wa mwani kutekeleza vema shughuli zao za kila siku .

Alisema kwasababu haiwezekani wanunuzi wa zao hilo wanaingia mikataba na wakulima lakini wanashindwa kutoa vifaa, kutokuwahudumia wala kutoa pembejeo kitendo ambacho kinapelekea wakulima kuhangaika bila kujua kamba wanatoa wapi.

“Hii haiwezekani mkulima wa mwani anakopa hii sio sawa unamuumiza mkulima kutokana na kwamba wanafanya kazi kubwa yenye tija lakini kama mkipata mwekezaji mzuri mtaweze kujikwamua kiuchumi nimewaelekeza Jiji na nitaongea na Waziri wa Uvuvi aweze kuona namna ya kuwasaidia tupate boti”Alisema

“lakini niwaambie wanunuzi kama hii kazi imewashinda tutavunja mikataba tuweze kujua wakulima wetu tunawahudumiaje tuwaitea mabenki waje watoe mikopo kama benki ya kilimo TIDB wanatoa mikopo yenye riba ndogo sana chini ya asilimia 4 mpaka 3waweze kuwakopesha waweze kununua kamba,taitai,troliki waweze kufanya kazi kwa tija yenye faida”Alisema

Aidha Mkuu huyo wa mkoa alisema Wizara ya Uvuvi watashirikiana nao kwenye suala la masoko huku akimpongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi Ulega kwa kuanzisha stakabadhi ghalani kama ilivyo mazao mengine ya kilimo .

Alisema mfumo huo utawezesha za la Mwani kuwekwa kwenye stoo utapigwa mnada na watapata bei ya soko kuliko ilivyokuwa bei ya sasa ambao madalali wanapanga bei wanayotaka jambo ambalo linawaumiza wakulima wengi.

“Nimetembelea Shamba la Mwana nimeona changamoto hawana vifaa vya kubebea mwani kutoka baharini mpaka nchi kavu ,hawana chombo wanatumia kama boya mpaka kufika pwani hiyo ni kazi kubwa ina tija hivyo nimewaekeza jiji nitaongoea pia na Waziri wa Uvuvi awasaidie mpate (faiba) boti hata ndogo milioni 15”Alisema

“Ndugu zangu hapa nimesikia mnachangamoto ya Kamba kazi hii bila kuwa navyo itakuwa ni ngumu hivyo nitawasaidia milioni 3 (3000, 000) kwa ajili ya kununua kamba taitai ili msimu utaoanza mwezi wa saba usipite bila kuwa nazo”Alisema RC huyo.

“Lakini lazima tuhakikishe kwanza tunakwenda na kauli mbiu ya Rais Dkt Samia Suluhu na Rais za Zanzibar Dkt Hussein Mwinyi ya uchumbi wa bluu kwa Mkoa wa Tanga tuliokuwa nao ni zao la mwani na ufungaji magongoo bahari na kwenda kwenye ufungaji wa pweza,kaa na majongoo bahari ,chaza,kamba”Alisema RC

Hata hivyo katika kuhakikisha analitilia mkazo zao hilo ,RC Batilda alisema kwamba Aprili 29 mwaka huu atakuwa na viongozi wa wavuvi na viongozi makampuni yanayonunua mwani ili kuweza kuweka mikakati ya namna ya kuweza kuhakikisha wakulima wanaendelea kupata tija. 

Hata hivyo Mkuu huyo wa mkoa alitumia wasaa huo kueleza kwamba vitu ambayo atasimama navyo ni kuhakikisha wanavidhibiti uvuvi haramu huku akiwaonya wanaojihusisha na uvuvi haramu kuachana nao.

About the author

mzalendo