Kimataifa

RAIS TUNUBU ATUMA WANAJESHI KUOKOA WANAFUNZI WALIOTEKWA

Written by mzalendo

Shambulio katika jimbo la Kaduna lilikuwa la pili la utekaji nyara wa watu wengi kwa kipindi cha wiki moja huko Nigeria

Rais wa Nigeria Bola Ahmed Tinubu siku ya Ijumaa alipeleka wanajeshi kuwaokoa zaidi ya wanafunzi 250 waliotekwa nyara na watu wenye silaha kutoka shule moja kaskazini-magharibi mwa nchi hiyo katika mojawapo ya utekaji nyara mkubwa zaidi katika miaka mitatu iliyopita.

Shambulio katika jimbo la Kaduna lilikuwa la pili la utekaji nyara wa watu wengi katika kipindi cha wiki moja katika nchi hiyo yenye watu wengi zaidi barani Afrika, ambapo magenge ya wahalifu wenye silaha wakiwa kwenye pikipiki wanawalenga waathirika katika vijiji na shule pamoja na barabara kuu wakidai kulipwa fidia.

Maafisa wa serikali wa eneo katika Jimbo la Kaduna walithibitisha kutokea kwa shambulio la utekaji nyara katika shule ya Kuriga siku ya Alhamisi, lakini hawakutoa takwimu kwani walisema bado wanachunguza ni watoto wangapi wametekwa nyara.

Mtu mmoja alipigwa risasi na kufa wakati wa shambulio hilo, wakaazi wa eneo hilo walisema. Sani Abdullahi, mwalimu wa shule ya GSS Kuriga katika wilaya ya Chikun, alisema wafanyakazi walifanikiwa kutoroka wakiwa na wanafunzi wengi wakati watu wenye silaha wanaojulikana kama majambazi walipowavamia Alhamisi na kurusha risasi hewani.

About the author

mzalendo