Featured Kitaifa

SERIKALI YAJIPANGA KUONGEZA KASI HAKI NA USAWA KIUCHUMI.

Written by mzalendo

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima,akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha Wakurugenzi wa Sera na Mipango kuhusu utekelezaji wa Ahadi za Nchi katika Kizazi Chenye Usawa kilichofanyika leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima,Akizungumza na Mwenyekiti wa Jukwaala Ushauri wa Kizazi Chenye Usawa na Waziri wa Maliasili Mhe. Angella Kairuki alipopiga simu kuongea na Waratibu wa Madawati ya jinsia kwenye Wizara na Wakurugenzi wa Mipango na Uratibu  leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii Mhe. Fatuma Towfiq,akizungumza wakati wa kikao kazi cha Wakurugenzi wa Sera na Mipango kuhusu utekelezaji wa Ahadi za Nchi katika Kizazi Chenye Usawa kilichofanyika leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Seif Shekalaghe,akizungumza wakati wa  kikao kazi cha Wakurugenzi wa Sera na Mipango kuhusu utekelezaji wa Ahadi za Nchi katika Kizazi Chenye Usawa kilichofanyika leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

 

Baadhi ya washiriki wakimsikiliza Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima (hayupo pichani) wakati akifungua kikao kazi cha Wakurugenzi wa Sera na Mipango kuhusu utekelezaji wa Ahadi za Nchi katika Kizazi Chenye Usawa kilichofanyika leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua kikao kazi cha Wakurugenzi wa Sera na Mipango kuhusu utekelezaji wa Ahadi za Nchi katika Kizazi Chenye Usawa kilichofanyika leo Februari 29,2024 jijini Dodoma.

Na WMJJWM, Dodoma

Serikali imewataka Wakurugenzi wa Sera na Mipango na Waratibu wa Madawati ya Kijinsia ndani ya Wizara zote kuongeza msukumo katika ajenda ya kumkomboa mwanamke kiuchumi, ambalo ni eneo lililoridhiwa na nchi katika mpango wa Jukwaa la Kizazi chenye Usawa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angella Kairuki ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri ya Kizazi chenye Usawa, wamewataka Watendaji hao kujipanga na kuhakikisha afua zinazotekelezwa ndani ya sekta zao zinatolewa taarifa kwa wakati.

Akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha utekelezaji wa Programu ya Jukwaa la kizazi chenye Usawa kwa Waratibu hao Februari 29, 2024 Jijini Dodoma, Waziri Dkt. Gwajima amewataka Wakurugenzi hao kutambua masuala yaliyowekewa Ahadi yanayohusisha sekta zao pamoja na kuratibu Afua zinazotekelezwa na kuzitolea taarifa kwa wakati.

Amewasisitiza kutambua Wadau waliopo kwenye maeneo yao na afua wanazotekeleza na kuwa na ripoti za matokeo chanya kwa sekta zao pamoja na kutambua Sera na Miongozo mbalimbali iliyopo na kuitumia kikamilifu.

“Natambua kuwa, kila Wizara imeteua Mratibu wa Programu hii katika eneo lake na kupewa jukumu la kusimamia utekelezaji. Nina Imani nanyi kuwa mtatimiza wajibu wenu kwa ufanisi mkubwa ili serikali chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan iendelee kugusa wananchi kiuchumi na kung’ara Kimataifa kama ahadi ilivyo.” amesisitiza Waziri Dkt. Gwajima.

Kwa upande wake Mhe. Angella Kairuki aliyeshiriki mkutano huo kwa njia ya simu akiwa safarini kikazi mkoa wa Tanga amesema, tangu nchi iridhie eneo la Haki na Usawa Kiuchumi mwaka 2021 imesalia miaka miwili kukamilisha utekelezaji
hivyo, lazima kama nchi kujitathmini hatua iliyofikiwa kwani ni shauku ya Mhe. Rais kuona kile alichokiridhia kinapata matokeo chanya.

“Nawasihi mkatenge Bajeti toshelevu kwa ajili ya kutekeleza afua za masuala ya kijinsia, kwani muda uliobakia ni mchache, lakini pia mhakikishe mnawasilisha taarifa za utekelezaji kwa muda ili itakapofika mwezi Mei tuone hatua tuliyoipiga” amesema Kairuki, kwa njia ya simu wakati wa ufunguzi wa kikao hicho .

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo na Ustawi wa Jamii Mhe. Fatuma Towfiq, akitoa salaam za Kamati, amesema imefika wakati sasa kwa Kamati hiyo kuzitaka Wizara zote kuwasilisha taarifa zake mbele ya Kamati hiyo, ili waweze kufanya tathmini ya miaka 20 baada ya Mkutano wa Bejing wa Mwaka 1995, ambapo Tanzania ilishiriki.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Seif Shekalaghe, amesema Wizara ya Maendeleo ya Jamii, ina jukumu la kuratibu shughuli za masuala ya jinsia kwa Wizara zote lakini nguvu yao itategemea zaidi utendaji wa wawakilishi wa Wizara za kisetka na uwasilishaji wa taarifa, hivyo ili Wizara hiyo iweze kutoa taarifa inayo jitosheleza kila Wizara haina budi kuwasilisha taarifa kwa wakati.

Tanzania iliwasilisha ahadi za Nchi ambazo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliahidi kuwa kinara katika utekelezaji wa eneo la Pili kuhusu Haki na Usawa wa Kiuchumi, katika Mkutano wa Kimataifa wa Jukwaa la Kizazi chenye Usawa, Jijini Paris – Ufaransa wa mwaka 2021.

About the author

mzalendo