Featured Kitaifa

PROF. MKENDA: WAMILIKI WA VIWANDA WAPENI NAFASI WAHITIMU WA FANI ZA SAYANSI NA TEKNOLOJIA KUONGEZA UMAHIRI WAO

Written by mzalendoeditor
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof Adolf Mkenda ametoa wito kwa wamiliki wa viwanda na sekta binafsi nchini kutoa fursa kwa wahitimu wa fani za Sayansi na Teknolojia ili kuwaongezea ujuzi na umahiri katika fani hizo.
 
Prof. Mkenda amesema hayo katika hotuba yake iliyosomwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe Leo tarehe 15, Disemba, 2023 katika mahafali ya 17 duru ya pili ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) Kampasi ya Mwanza.
 
Prof. Mkenda amesema,ili vijana wetu wanaohitimu leo wajifunze kwa vitendo lazima waende viwandani wajifunze kwa vitendo naomba nitoe wito wangu kwa sekta binafsi mtusaidie kuondoa obwe lililopo tunapowatafutia maeneo ya kujifunza kwa vitendo muwachukue ili wajifunze zaidi kwa maendeleo ya uchumi wao na Taifa kwa ujumla.
 
Aidha, Katika Mahafali hayo wanafunzi 68 wamehitimu katika ngazi ya Staashada na Astaashahada katika fani mbali mbali ikiwemo fani ya Tekenolojia ya Ngozi na Sayansi ya Maabara.
 
Prof. Mkenda amesema wahitimu hawa wanakwenda kuonaongeza idadi ya mafundi sanifu katika soko la ajira,na wanakwenda kuiwezesha nchi kuwa na rasilimali watu wa kuchachua maendeleo na kufikia ndoto kubwa ambazo taifa linazo katika kutatua changamoto mbalimbali za ndani ya jamii.
“Mkiwa sasa ni wahitimu wa ufundi sanifu, bila shaka mnatambua hazina kubwa ya elimu ya ufundi sanifu mliyoipata. Nina imani mtatumia hazina hiyo kwa manufaa yenu binafsi, familia zenu na taifa letu kwa ujumla,” amesema Prof. Mkenda.
Amesema serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuongeza fursa za mafunzo na elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi nchini na kusimamia ubora wa elimu.
 
Aidha, ameongeza, serikali pia imeendelea kuwajengea uwezo watumishi katika taasisi za elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi nchini, ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu.
Naye mkuu wa Taasisi ya Tekenolojia Dar es Salaam (DIT), Prof. Preksedis Marco Ndomba amesema idadi ya wahitimu wa kike wanaohitimu leo ni sawa na asilimia 37, na DIT inajivunia kuendelea kuongeza asilimia ya wahitimu wa kike mwaka hadi mwaka.
 
“Kwa mfano, miaka mitatu iliyopita asilimia ya wahitimu wa kike ilikuwa 30. Haya ni matunda ya hamasa kubwa tunayoendelea kuifanya mikoa yote ya Tanzania na tunaamini asilimia hii itaendelea kupanda mwaka hadi mwaka.
“Hapa mbele kuna wahitimu wengine wa kozi ya ufundi stadi katika fani ya usaidizi wa maabara, bidhaa za ngozi na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA). Idadi ya wahitimu wa kike ni sawa na asilimia 39,” amesema Prof. Ndomba.
 
Hata hiyo mgeni rasmi amehitimisha kwa kuiomba menejimenti ya DIT kuwa na mkakati maalum wakuhamasisha mabinti kujiunga na masomo ya sayansi na Teknolojia kwakuwa tayali serikali imeboresha miundombinu ya majengo kupitia fedha za mkopo wa Benki ya Dunia, kupitia mradi wa (EASTRIP) unaoendelea katika kampasi ya Mwanza.

About the author

mzalendoeditor