Featured Kitaifa

WAZIRI NDALICHAKO ATOA RAI KWA WANANCHI WA MTWARA KUCHANGAMKIA FURSA ZA KIBIASHARA

Written by mzalendoeditor

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu) Prof.Joyce Ndalichako ametoa rai kwa wananchi wa Mtwara kuzichangamkia fursa za kibiashara zilizopo mkoani humo ili kukuza uchumi.

Ndalichako amesema hayo Mkoani Mtwara wakati akifungua maonesho ya biashara,Uwekezaji na fursa yanayofanyika katika viwanja vya mashujaa kuanzia Machi 19 hadi Machi 31,mwaka huu.

Amesema kuwa Mkoa huo unakuwa kwa kasi kiuchumi hivyo ni vyema kila mwananchi akatambua kuwa hiyo ni fursa katika kukuza uchumi kibiashara.

“Maonesho haya ya Biashara, Uwekezaji na Fursa ni maonesho ya Kwanza kufanyika Mkoani Mtwara yakiwa na lengo la kuwaleta pamoja wadau mbalimbali katika Sekta hiyo ili kubadilishana uzoefu wa kitaalamu na kujifunza biashara na uwekezaji wa kisasa pamoja na fursa zilizopo katika sekta hiyo na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla,”amesema Ndalichako.

Aidha Ndalichako alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wananchi katika uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru utakaowashwa Aprili 1 mwaka huu katika kiwanja cha Nangwanda sijaona,Mkoani hapo.

Akizungumza na Vyombo ya habari Kaimu Afisa Mfawidhi wa TASAC Mkoa wa Mtwara katika maonesho hayo Mha. Joseph Myaka amesema kuwa katika kutekeleza majukumu yao Shirika hilo limejikita katika kutoa elimu kwa wananchi kufahamu shirika hilo linavyotekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria.

Amesema kuwa licha ya majukumu makubwa waliyonayo pia TASAC imeshiriki maonesho hayo ili kuwapa elimu wananchi kuhusu fursa za biashara zilizopo katika Sekta ya Usafiri kwa njia ya Maji sambamba na elimu kuhusu Usalama, Ulinzi na Utunzaji wa mazingira majini jukumu linalotekelezwa na Shirika hilo.

“TASAC tunashiriki maonesho haya ya Biashara Uwekezaji na Fursa mkoani Mtwara ili kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yanayotekezwa Kisheria kama mdhibiti wa shughuli za usafiri kwa njia ya maji tunasimamia huduma zinazotolewa na Bandari, tunadhibiti na kusimamia ulinzi, usalama na utunzaji wa mazingira na kuratibu shughuli za uokoaji na utafutaji pale panapotokea dhoruba majini,

“Pia tunatoa elimu kwa wananchi wa Mtwara na wadau wa usafiri kwa njia ya maji katika jukumu letu la Udhibiti wa Safari kwa njia ya Maji na udhibiti Usalama, Ulinzi na Utunzaji wa Mazingira majini, wanaweza kufanya shughuli zao kwa usalama na kupata maendeleo na kuongeza pato la Taifa,”ameeleza Myaka.

Aidha ameeleza kuwa kwa mujibu wa Sheria, TASAC ina wajibu wa kusimamia kazi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhimiza usimizi na shughuli za uwakala wa meli wenye ufanisi, kuhimiza shughuli za bandari na huduma za meli zenye ufanisi, kuhakikisha kunakuwepo usalama na ulinzi wa shehena, kuhimiza na kutunza mazingira, usalama na ulinzi wa bahari, maziwa na mito.

About the author

mzalendoeditor