Featured Kitaifa

WAZIRI MKUU AKAGUA UWANJA WA NDEGE WA TERMINAL 1

Written by mzalendoeditor

Waziri Mkuu Kassim akizungumza Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala la Ndege za Serikali (TGFA) John Nzulule, wakati alipotembelea karakana ya Wakala wa Ndege za Serikali, Machi 28, 2023 jijini Dar es salaam. Katikati ni Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete.  

Waziri Mkuu Kassim akizungumza na Viongozi wa Serikali pamoja na Watumishi wa Wakala la Ndege za Serikali (TGFA), wakati alipotembelea karakana ya Wakala wa Ndege za Serikali, Machi 28, 2023 jijini Dar es salaam. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekagua uwanja wa ndege wa Terminal I ili kujiridhisha na kazi ya ukarabati unaoendelea kwenye eneo la kuegesha na kufanyia matengenezo ya ndege za Serikali.

Pia amewataka viongozi na wafanyakazi wa Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA) wahakikishe wanashirikiana na mamlaka husika kuufanya uwanja huo wakati wote unakuwa nadhifu ili kukidhi hadhi ya viongozi wa kitaifa na kimataifa wanaoingia ama kuondoka nchini.

Akizungumza na viongozi na watumishi wa TGFA mara baada ya kufanya ukaguzi huo leo (Jumanne, Machi 28, 2023) jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa TGFA, Mhandisi John Nzulule ahakikishe ujenzi huo unakamilika haraka.

“Serikali ilishatoa kibali kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa karakana hiyo ambayo nimeelezwa itakapokamilika itawezesha kuegesha ndege kubwa mbili kwa wakati mmoja  pale zinapohitaji matengenezo.”

Pia amewaagiza Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwan Kikwete na Katibu Mkuu wa Utumishi, Bw. Juma Mkomi wafuatilie maslahi na motisha za watumishi wa taasisi hiyo ili kuinua ari yao ya utendaji kazi.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na watumishi hao, Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwan Kikwete alimweleza Waziri Mkuu kwamba Serikali ilitoa sh. bilioni 2.5 za ujenzi wa awamu ya kwanza ya ofisi za TGFA ambao umekamilika na ofisi zimeanza kutumika.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa TGFA, alisema kukamilika kwa jengo hilo kumesaidia kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa idara zilizopo uwanja wa ndege kwa kuwa lina nafasi za kutosha na mifumo ya kisasa kwa ajili ya marubani, wahandisi, wahudumu wa ndege na watumishi wengine.

Alisema awamu ya pili ya ujenzi inahusisha ujenzi wa eneo la kuegesha na kufanyia matengenezo ya ndege na inatarajiwa kuanza hivi karibuni kwa sababu kibali cha ujenzi kimeshapatikana.

“Taratibu za kumpata mkandarasi zimeshakamilika na taratibu zote za kimkataba zimekamilika. Tunaahidi kusimamia kazi hii ili kupata thamani halisi ya fedha (value for money) katika mradi huu,” alisema.

About the author

mzalendoeditor