Featured Kitaifa

MAONESHO YA MADINI YAWANUFAISHA WACHIMBAJI CHUNYA

Written by mzalendoeditor

Wachimbaji na wananchi wa Mkoa wa Kimadini Chunya wamenufaika kwa elimu iliyotolewa na kujifunza mengi kutoka kwa taasisi, kampuni na wadau mbalimbali wa sekta ya Madini.

Hayo ameyasemwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Zuberi Homera katika kilele cha Maonesho ya Kwanza ya Teknolojia ya Madini Mkoa wa Mbeya yanayofanyika katika viwanja vya Sinjiriri katika Mkoa wa Kimadini Chunya.

Homera amesema wachimbaji na wananchi waliofika katika maonesho hayo wamejifunza namna bora ya matumizi sahihi ya utendaji kazi wa mitambo mbalimbali pamoja na njia nzuri za uchimbaji madini na aina za madini yanayopatikana katika mkoa wa Mbeya.

Aidha, Homera ameitaka Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mbeya kuhakikisha inaendelea kulinda na kusimamia rasilimali madini na kuwahasa wananchi kuwafichua wote wenye tabia ya kutorosha madini.

Pia, Homera ametumia maonesho hayo kuzindua mtambo uliyonunuliwa na mchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu Malulu Shimba kutoka kwa kampuni za Appolo Heavy Equipment kiasi cha Shilingi milioni mia tatu na ishirini (375,000,000).

Naye, Mwenyekiti wa Wachimbaji Madini wa Mkoa wa Mbeya (MBELEMA) Leonard Manyesha ameiomba Serikali kufanya maonesho hayo kuwa endelevu kwa kila mwaka na yakusanye wachimbaji wengi zaidi wa mkoa wa Mbeya.

Katika hatua nyingine, Manyesha ameziomba taasisi za fedha kuwatambua wachimbaji wadogo kwa kuwakopesha na kupunguza masharti ya mikopo sambamba na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Halmashauri ya Wilaya hiyo kupunguza tozo na ushuru ili kuleta ufanisi katika kazi zao.

About the author

mzalendoeditor