Featured Kitaifa

RAIS SAMIA ATOA WITO KWA WANAWAKE KUSHIKAMANA

Written by mzalendoeditor
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Maridhiano kutoka kwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mhe. Freeman Mbowe aliyeikabidhi kwa niaba ya Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) mara baada ya kuwahutubia kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Moshi Mkoani Kilimanjaro tarehe 08 Machi, 2023.
 viongozi mbalimbali wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) pamoja na Wanachama wa Chama hicho wakishangilia wakati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akiwahutubia katika Mkutano wa Baraza hilo uliofanyika Moshi mkoani Kilimanjaro katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) pamoja na Wanachama wa Chama hicho kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Moshi Mkoani Kilimanjaro tarehe 08 Machi, 2023.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mhe. Freeman Mbowe, pamoja na viongozi mbalimbali wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) mara baada ya kuwahutubia kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Moshi Mkoani Kilimanjaro tarehe 08 Machi, 2023.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ametoa wito kwa Baraza la Wanawake wa Chadema (BAWACHA) kutumia nguvu ya Chama chao kuungana na kila chama cha siasa kumkomboa mwanamke wa Tanzania.  

Rais Samia amesema hayo wakati akihutubia katika Kongamano la Siku ya Wanawake Duniani lilioandaliwa na BAWACHA katika Ukumbi wa Kuringe.  

Aidha, Rais Samia amesema lengo ni kuona mwanamke wa kitanzania anathaminiwa na kupewa haki kama mwingine yeyote duniani kwa kuwa changamoto hazichagui dini, kabila wala itikadi ya kisiasa.

Rais Samia pia amewataka wanawake kutumia siku hii kutathmini maendeleo ya wanawake na changamoto wanazokabiliana nazo kisiasa, kiuchumi na kijamii ili kupata maridhiano ya haki zao katika usawa wa kijinsia.

Vile vile, Rais Samia amevitaka vyama vya siasa kufanya kazi kwa pamoja na kushikamana ili kukuza siasa za kistaarabu na za kusikilizana zitakazoleta heshima kwa taifa na kustawisha uchumi.

Rais Samia pia amesema alitumia ubunifu kuunganisha taifa kwa kuhakikisha kunakuwa na maridhiano na uvumilivu ili kuleta mageuzi ambayo yameweka msingi mzuri katika mustakbali wa demokrasia na maendeleo ya taifa letu.

Kwa upande mwingine, Rais Samia alitembelea ofisi za Chama cha Mapinduzi (CCM) na kuzungumza na Uongozi wa Mkoa pamoja na wanachama wa mkoa wa Kilimanjaro.

About the author

mzalendoeditor