Featured Kimataifa

MAKAMU WA RAIS ATETA NA WATANZANIA WAISHIO AZERBAIJAN

Written by mzalendoeditor

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akifanya mazungumzo na  mazungumzo na watanzania waishio nchini Azerbaijan, Mazungumzo yaliofanyika katika Jiji la Baku nchini humo leo tarehe 02 Machi 2023.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango  akiwa na Balozi wa Tanzania nchini Urusi Mheshimiwa Fredrick Kibuta katika picha ya pamoja na baadhi watanzania waishio nchini Azerbaijan mara baada ya mazungumzo  yaliofanyika katika Jiji la Baku nchini humo leo tarehe 02 Machi 2023.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 02 Machi 2023 amekutana na kufanya mazungumzo na watanzania waishio nchini Azerbaijan, Mazungumzo yaliofanyika katika Jiji la Baku nchini humo.

Akizungumza na Watanzania hao, Makamu wa Rais amewaasa watanzania hao kuendelea kuitangaza vema Tanzania na vivutio vyake vilivyopo,kutangaza lugha ya Kiswahili na kuendelea kueneza utamaduni wa Tanzania pamoja na kuwa wazalendo kwa nchi yao.

Pia amewaagiza kutoa elimu kwa watanzania wengine juu ya fursa za elimu zilizopo katika jumuiya yan chi wanachama zisizofungamana na upande wowote.

Makamu wa Rais amewataka watanzania waishio nje ya Tanzania kufuata sheria na taratibu za nchi walizopo pamoja na kujifunza mazuri katika nchi hizo na kuhamishia maarifa hayo nchini Tanzania.

Pia amewaasa kutambua jukumu la kwanza la ujenzi wa Tanzania litafanywa na watanzania wenyewe hivyo wanapaswa kutoa mchango wa kila hali katika kuliletea taifa maendeleo.

Amesema serikali itaendelea kuleta mabadiliko yenye tija kwa watanzania wote ikiwemo kuendelea na jitihada za kuboresha sekta mbalimbali kama vile Afya, Elimu na Miundombinu pamoja na hivi sasa kuanzisha programu maalum ya kilimo ya Building Better Tomorrow itakayowasaidia vijana katika sekta hiyo.

Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Urusi Mheshimiwa Fredrick Kibuta.

Makamu wa Rais yupo nchini Azerbaijan kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (Non-Aligned Movement) unaojadili kuhusu namna ya kukabiliana na athari za Uviko-19.

About the author

mzalendoeditor