Featured Kitaifa

SPIKA DKT. TULIA AWAASA WABUNGE WA EAC KUTUMIA MASHINDANO YA KILA MWAKA YA KIMICHEZO KUENDELEZA UMOJA

Written by mzalendoeditor

 

Spika wa Bunge,  Dkt. Tulia Ackson, akizungumza wakati wa hafla ya ufungaji wa Mashindano ya 12 ya michezo ya Wabunge wa Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Jijini Juba nchini Sudan Kusini.

……………………………..

 Na Mwandishi Maalum, Juba Nchini Sudan Kusini

Spika wa Bunge, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson amewaasa Wabunge wa Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kudumisha kauli mbiu  ya Mashindano ya kila mwaka ya kimichezo ya Mabunge hayo ambayo ni ‘Kupanua na Kuimarisha Muungano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki’.

Akizungumza wakati wa hafla ya ufungaji wa Mashindano ya 12 ya michezo hiyo  Jijini Juba nchini Sudan Kusini, Dkt. Tulia alisema ni lazima kauli mbiu ya Mashindano hayo iendelee kudumishwa ili iweze kuleta matokeo chanya katika kusaidia Jumuiya ya Afrika Mashariki kuendelea kuwa na umoja. 

“Kauli mbiu ya Mashindano haya lazima iendelee kudumishwa, hatujaja kushidana bali kujenga umoja wa Jumuiya yetu,” alisisitiza Spika Dkt. Tulia.

Aliongeza kuwa kuwepo kwa rufaa nyingi baina ya  timu na timu katika Mashindano hayo kunaonesha kwamba kuna tatizo.  

“Tunapoona rufaa nyingi inaashiria kuna tatizo na hivyo ni lazima tubadilike hatuwezi kushiriki Mashindano haya wakati tunaendelea kudanganyana,” alisema Dkt. Tulia Ackson.

Mbali na hayo, Dkt. Tulia alisititiza pia kwamba lazima sheria za  Mashindano hayo ziheshimiwe  ili kusonga mbele.

“Mashindano haya si Kombe la Dunia ni kwa ajili ya kujuana na kudumisha umoja wetu,” alisema Dkt. Tulia na kuongeza kwamba; kwa rufaa  na  udanganyifu unaojitokeza wakati wa Mashindano hayo, malengo  ya kujenga Jumuiya imara hayawezi kufikiwa.

Kwa upande mwingine, Spika Dkt  Tulia aliishukuru Sudan Kusini kwa kuandaa Mashindano hayo na kipekee kuipongeza  kwa kufanya vizuri ingawa ni nchi changa na ngeni.

“Tutatangaza tulichoona mnafanya vizuri, hongereni sana,” alisema.

Spika Dkt. Tulia aliongeza pia Sudan Kusini kwa jinsi walivyohamasisha wananchi kufika viwanjani kushuhudia Mashindano hayo.

“Mashindano haya si kwa ajili ya Wabunge tu, ni kwa ajili ya wananchi hivyo  nawapongeza Sudan Kusini kwa sababu wanachi walijitokeza kwa wingi kushuhuhudia Mashindano haya,” alisema.

Spika Dkt. Tulia alihitimisha kwa kuwaambia washiriki wa Mashindano hayo kurudi katika nchi zao na ujumbe kwamba Sudan Kusini kuna amani tele tofauti na jinsi ambavyo imekuwa ikisikika.

About the author

mzalendoeditor