Featured Kitaifa

WADAU WA NISHATI NCHINI WAKUTANA KUJADILI MPANGO WA MATUMIZI BORA YA NISHATI KWENYE MAJENGO

Written by mzalendoeditor
 
Shirika la Umoja la Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP) kwa kushirikiana na Wizara ya Nishati imeandaa warsha ya siku mbili ya wadau wa nishati kutoka Wizara ya Nishati, Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, EWURA, TANESCO, Baraza la Taifa la Ujenzi, na TAMISEMI yamefanyika Bagamoyo kuanzia 25-26 Novemba 2022 kujadili namna bora ya matumizi bora ya nishati nchini. 
 
 
Mradi huu wa Mpango wa Matumizi Bora ya Nishati Tanzania unafadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na kutekelezwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Shirika la Umoja aa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP).  
     
 
‘Mratibu wa mradi wa Mpango wa Matumizi Bora ya Nishati Tanzania, Bwana Aaron Cunningham alisema “warsha hii imekusudia kujadili majukumu ya washikadau katika kutekeleza na kuendeleza matumizi bora ya nishati katika majengo, kwa kushirikiana na Baraza la Ujenzi la Taifa tumekusudia kushirikiana na wizara ya ujenzi kuandaa mfumo wa matumizi bora ya nishati katika majengo makubwa. 
 
 
Aliongeza kwa kusema ‘mpango huu wa uundaji na uendelezaji wa majengo yenye kuzingatia matumizi bora ya nishati yatasaidia kupunguza matumizi yasiyosahihi ya nishati na kuokoa fedha pamoja na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya Tabianchi.” – Aaron Cunningham, UNDP. 
 
Ripoti ya nishati Tanzania ya mwaka 2018 inaonyesha nishati kwa kiasi kikubwa inatumika kwenye majengo ya biashara, makazi ya watu na viwandani. Mpango kazi wa taifa wa nishati umetambua sekta ya majengo kama sekta muhimu kwenye kupunguza matumizi yasiyo sahihi ya nishati.  
 
 
Nae mkurugenzi wa huduma za kiufundi kutoka baraza la Taifa la Ujenzi, Mhandisi Moses Lawrence alisema ‘Wizara ya ujenzi na uchukuzi ipo kwenye mchakato wa kuandaa sheria ya ujenzi wa majengo (building act and building codes) ambapo itazingatia nishati bora na endelevu na hivyo kuwataka wadau kutoa michango ya mawazo ili kufanikisha mchakato huu.
 
 Mradi wa Mpango wa Matumizi Bora ya Nishati Tanzania unaotekelezwa na UNDP kwa kushirikiana na Wizara ya Nishati utangalia na kuzingatia namna bora ya kushirikiana na Baraza la Taifa la Ujenzi kufanikisha malengo haya.
 
 
Mhandisi Moses aliongeza kwa kusema uzingatiaji wa matumizi bora ya nishati kwenye majengo katika hatua za mwanzo za ujenzi ni wa gharama nafuu zaidi kuliko uboreshaji baada ya ujenzi. Kwa hiyo, maamuzi yaliyofanywa hatua za mwanzo za ujenzi wa jengo yataamua matumizi ya baada ya jengo kukamilika. – Eng. Moses Lawrence.
 
 
Ujenzi wa kuzingatia matumizi bora ya nishati utasaidia kubadilisha sekta ya ujenzi kuwa mazingira rafiki, gharama nafuu, na matumizi bora ya nishati. Kama matokeo ya muda mrefu, kanuni za ujenzi wenye kuzingatia matumizi bora ya nishati zitachangia lengo la 7 la Maendeleo Endelevu (SDGs) ambalo linahusu nishati safi na himilivu (Affordable and Clean Energy) kwa wote, na lengo la 13 linalohusu hatua za kuchukuwa kupambana na mabadiliko ya tabianchi (Climate Action) ambalo linalingana na vipaumbele vya maendeleo vya kitaifa.
 
 
Mpango wa matumizi bora ya nishati katika sekta ya ujenzi utasaidia juhudi za serikali za kutoa nishati ya kutosha na ya uhakika, hususani umeme, ili kukidhi ongezeko la mahitaji. Pia itaongeza ufahamu wa watumiaji kuhusu manufaa ya majengo yenye kufuata kanuni za ujenzi na matumizi bora ya nishati.

About the author

mzalendoeditor