Featured Kitaifa

WAZIRI MKENDA ATOA ONYO KWA BODI YA MIKOPO KUTOTOA USHIRIKIANO KAMATI YA UCHUNGUZI UTOAJI MIKOPO

Written by mzalendoeditor

Na Mathias Canal, WEST-Dar es salaam

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda ametoa onyo kwa uongozi wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kutokana na kitendo cha Bodi hiyo kwa kutotoa ushirikiano kwa kamati ya kuchunguza utoaji wa mikopo.

Waziri Mkenda ametoa onyo hilo jana tarehe 25 Octoba 2022 wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es salaam na kusema kuwa Bodi inasuasua kutoa ushirikiano kwa kamati aliyoitangaza tarehe 31 Julai mwaka huu alipotembelea ofisi za Bodi hiyo maeneo ya Tazara Jijini Dar es salaam.

Waziri Mkenda ameeleza kuwa majukumu aliyoyatoa kwa kamati hiyo ilikuwa ni kuchunguza uhalali katika utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2017/2018 mpaka 2021/2022 ili kubaini kama kulikuwa na upendeleo wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wasiokuwa na sifa zilizoainishwa.

Prof. Mkenda amesema kuwa atakula kichwa cha mtu kama Bodi ya Mikopo itaendelea kusuasua katika utekelezaji wa kazi hiyo. “Mara wapite huku mara watokee huku Lengo la timu hii tungependa kile kidogo tulichonacho kitolewe kwa haki kusaidia wale wenye mahitaji makubwa zaidi” Amekaririwa Prof Mkenda

“Lakini pia kuhakikisha kwamba hakuna fursa ya mimi waziri, mtoto wangu au ndugu zangu wenye uwezo kuhakikisha wao wanapata kwa sababu wao wana connection wakati mtu ambaye hana connection hapati,” amesisitiza

Waziri Mkenda ameonyesha masikitiko yake dhidi ya Bodi ya Mikopo (HESLB) na kueleza kuwa kamati hiyo imechelewa kufanya kazi yake kwa sababu ya ‘lobbying’ (inashawishi) huku na kule ilihali wakifahamu kwamba kamati ya waziri haisimamishwi kufanya kazi.

“Wasi-lobby na bodi ya mikopo nitawachukulia hatua wakiendelea kufanya lobby-lobby kwa sababu wanataka kutuambia na wenyewe wanataka kuficha mambo, Ile kamati ifanye kazi, taarifa ni yetu tutaifanyia kazi kwa ndani kwa sababu sisi hatulengi kwenda kumuumbua sijui mtoto wa Salum amepata mkopo hapana” Amesema Waziri Mkenda na kuongeza kuwa

“Sisi tunataka kujisahihisha ili kuhakikisha kwamba kile ambacho serikali imetenga kwa ajili ya mikopo kwa wanafunzi kinaenda kwa mlengwa, sasa ninataka kutoa onyo ya kwamba kwenda kulobby sijui eti waziri asimamishe kamati isifanye kazi… hiyo lobbying inaonesha kuna madudu,”

“Natuma salamu kwa bodi ya mikopo kwa sababu niliona wamejaribu wanasema ooh tumeitwa sijui tumetuma tusimamishe wakati kazi nimeitoa mimi na mimi ndio nimepewa kazi ya kusimamia mikopo.

“Bungeni watu wanalalamika sana, wanasema kuna yatima hawapewi mikopo, alafu watu wenye uwezo wanapewa mikopo, mimi naunda kamati alafu nisikie kuna mtu anasema waziri asiunde kamati, aah! Nitakula kichwa cha mtu,” Amesisitiza

Kamati hiyo ya kufuatilia utoaji wa mikopo kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2017/2018 mpaka 2021/2022 aliyoitangaza Waziri Mkenda, inaongozwa na Profesa Allan Mushi ambaye ni mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe Morogoro, Idd Makame kutoka Zanzibar na Dk. Martin Chegeni ambao wote kwa pamoja ni wataalamu wa mifumo waliobobea katika sayansi ya kompyuta na takwimu.

About the author

mzalendoeditor