RAIS wa Urusi Vladimir Putin ameishushia lawama nchi ya Ukraine kwa kuvamia na kuharibu miundombinu ya daraja la Kerch linalounganisha kati ya Urusi na eneo la Crimera ambalo limechukuliwa na nchi hiyo.
Daraja hilo ambalo limebeba ishara kubwa ya urithi wa Urusi pamoja na kuwa eneo muhimu kimkakati linasadikiwa kuvunjwa kwa kutumiwa kile kinachoitwa na Moscow kuwa ni bomu lililokuwa limepandikizwa kwenye gari la mizigo.
“Hapana shaka hiki ni kitendo cha kigaidi ambacho kimedhamiria kuharibu miundombinu ya raia.” Alisema Putin siku ya jumapili katika video ambayo ilichapishwa na Ikulu ya Kremlin kupitia mtandao wa Telegram.
Putin ameendelea kwa kudai kuwa kile kilikuwa ni kifaa kilichobebwa na kutumwa na vikosi maalum vya Ukraine.
Siku ya Jumatatu (leo), Rais Putin anatarajia kuitisha Baraza la Usalama la Taifa ambalo Makamu Mwenyekiti wake ni Rais wa zamani wa nchi hiyo Dmitry Medvedev ambaye amebainisha kuwa gaidi aliyehusika katika shambulio hilo anatakiwa kuuawa mara moja.
“Urusi inaweza kujibu mashambulizi kwa matukio kama haya kwani mhusika wa tukio hili anatakiwa kuuawa mara moja kitu ambacho ni utamaduni wa maeneo yote duniani. Hiki ndicho wananchi wa Urusi wanachotarajia.” Alinukuliwa Rais huyo wa zamani akiongea na Shirika la Habari la Tass.