Featured Kitaifa

YALIYOJIRI KATIKA TAMASHA LA JINSIA KANDA YA KASKAZINI 2022

Written by mzalendoeditor

Rose Mwalongo Ngunangwa akiwasilisha taarifa ya mambo yaliyojiri kwa niaba ya TGNP wakati wa Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini Ijumaa Oktoba 7,2022 lililofanyika kwa muda wa siku tatu (Oktoba 5-7,2022) katika viwanja vya Kwasa Kwasa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro Mhe. Edward Mpogolo akizungumza wakati akifunga Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini  Ijumaa Oktoba 7,2022 lililofanyika kwa muda wa siku tatu (Oktoba 5-7,2022) katika viwanja vya Kwasa Kwasa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi  akizungumza wakati wa kufunga Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini Ijumaa Oktoba 7,2022 lililofanyika kwa muda wa siku tatu (Oktoba 5-7,2022) katika viwanja vya Kwasa Kwasa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro.

 

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu akifurahia jambo na washiriki wa Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini.

 

 

 

TAARIFA
KWA UMMA

Yaliyojiri
katika Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini

Tarehe
5-7 Oktoba 2022, Wilaya ya Same, Kilimanjaro
 

“Haki
ya Uchumi: Rasilimali Ziwanufaishe Wananchi Walioko Pembezoni”

 

Kuanzia tarehe 5 Oktoba
hadi 7 Oktoba 2022
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)
kwa kushirikiana na mashirika mbalimbali yanayotetea haki za wanawake na usawa
wa jinsia, wanaharakati binafsi na kwa ufadhili wa Ubalozi wa Watu wa Kanada,
na Uswidi, umefanya Tamasha la Jinsia la Kanda katika Viwanja vya Kwasa
Kwasa hapa Wilayani Same, Mkoani Kilimanjaro.

 

Tamasha la Jinsia la Kanda limeongozwa
na mada kuu isemayo,
Haki ya Uchumi: Rasilimali
Ziwanufaishe Wananchi Walioko Pembezoni
’, huku mada ndogo ndogo zikiangazia
fursa za kilimo, uongozi shirikishi, mila kandamizi, huduma za kijamii (afya ya
uzazi), na ujenzi wa nguzu za pamoja yaani TAPO.

 

Tamasha la Jinsia la Kanda
limekutanisha zaidi ya washiriki 500 wanaojumuisha wadau wa maendeleo (Ubalozi
za Uswidi, Ubalozi wa Canada, Global Affairs Canada, Chuo cha Coady,
SeedChange, Crossroads International,
Aga Khan Foundation, ONGAWA
), sekta binafsi, asasi za kiraia, vikundi
vya kijamii na wanaharakati ambao wamekuwa bega kwa bega na TGNP katika
kuchagiza usawa wa jinsia. Serikali ya Jamhuri ya Tanzania imeshiriki kupitia TAMISEMI
na Wizara ya Maendeleo ya Jamii.

 

Mkurugenzi wa TGNP, Bi. Lilian Liundi
kwa niaba ya Bodi ya Wakurugenzi na Wanachama alitoa usuli kuhusu Tamasha la
Jinsia la Kanda ikiwa ni muendelezo wa mkakati wa taasisi tokea mwaka 1996 kuunganisha
sauti ya pamoja na kutekeleza mikakati ya kufikia usawa wa kijinsia. TGNP
imefanya matamasha 14 kitaifa na katika ngazi ya wilaya kwa mafanikio makubwa
ya kufikia washiriki 31,000 (70% wanawake na 30% wanaume) na kushawishi
mabadiliko. Hivyo, Tamasha limekuwa sehemu
ya kuendelea kutanua harakati za ujenzi wa nguvu za pamoja nchini na kutoa
fursa kwa watu wengi zaidi kushiriki.

 

Mgeni Rasmi wa Tamasha la Jinsia la
Kanda, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mheshimiwa Nurdin Babu katika neno la
ufunguzi alitambua mchango wa TGNP katika kuwainua wanawake kiuchumi na
kuongeza ushiriki wao kwenye nafasi za uongozi na ngazi za maamuzi.

 

Aidha, akipinga ukatili wa kijinsia
mkoani Kilimanjaro, Mheshimiwa Nurdin Babu aliweka wazi nia ya dhati
kukomesha vitendo vya ukatili kwa kuelekeza wananchi kufika ofisini kwake bila
kusita
. Aidha, alitoa maelekezo kwa Mkuu wa Wilaya ya Same kuwasilisha
Agenda ya Masoko kwa Wanawake Wakulima wa Tangawizi kwenye Mkutano wa Baraza la
Biashara la Mkoa
lililopangwa kufanyika tarehe 6 Oktoba 2022. 

 

Pia kuunga
mkono jitihada za wanawake, vijana na watu wenye ulemavu,
ameelekeza Ofisi
ya Mkurugenzi wa Halmshauri ya Wilaya ya Same kuendeleza utoaji wa mikopo,
kuondoa urasimu, na kuongeza kiwango cha mikopo hiyo ili kuwakwamua kiuchumi
.

 

Katika siku ya pili ya Tamasha,
washiriki walijikita kwenye tafakuri na mijadala kupitia warsha zilizoangazia
maeneo muhimu manne (4): Haki ya Uchumi; Huduma za Kijamii (Afya ya Uzazi);
Uongozi Shirikishi; na Mila Kandamizi. 

 

Kwa ujumla, changamoto zilizotambuliwa
katika maeneo hayo ni pamoja na upatikanaji na urasimu kufikia mikopo na mitaji
ya biashara kwa wanawake, ukosefu wa masoko na bei za uhakika kwa mazao kama
tangawizi, uhaba wa taarifa juu ya afya ya uzazi, sheria kandamizi kwa wajane
na Watoto wa kike, na ukatili wa kijinsia unaohusihwa na mila potofu.

 

Pamoja na kutambua na kuchambua
changamoto nyingi zilizopo kwenye jamii zao, washiriki walifanikiwa kutoa
mapendekezo makuu ya utatuzi kama ifuatavyo:

·       Kuboresha mfumo na utaratibu wa utoaji wa mikopo ya Halmashauri
na mafunzo ya uendeshaji miradi/biashara na utunzaji wa fedha kwa wanawake,
vijana na makundi mengine ili kupunguza urasimu na kuwezesha upatikanaji rahisi
wa taarifa kuhusu fursa kwa makundi hayo.

 

·       Halmashauri ya Wilaya, hususani, maafisa biashara kwa
kushirikiana na sekta binafsi na taasisi zisizo za kiserikali kuwapatia taarifa
(kupitia teknolojia ya simu) na kuwajengea uwezo wanawake na makundi mengine ya
pembezoni wanaoshiriki katika kilimo kutambua na kufikia masoko na kunufaika na
bei nzuri kwa mazao yao.

 

·       Wajumbe wa Kamati za Vijiji kuweka hamasa na kutumia fursa
mbalimbali za kujiongezea uwezo na uelewa kuhusu elimu ya afya ya uzazi ili
kuwa mstari wa mbale katika kusimamia kwa ufanisi wa utoaji huduma hizo.

 

·       Serikali za Vijiji kwa kupitia Utaratibu uliowekwa na TAMISEMI
wa Fursa na Vikwazo vya Maendeleo (yaani O&0D) kutambua na kuweka kuwa
kipaumbele upatikanaji wa vifaa tiba na idadi ya kutosha ya watoa huduma kwenye
zahanati na vituo vya afya.

 

·       Kuchagiza mapitio na marekebisho ya sheria (Uchaguzi Serikali za
Mitaa) na Kanuni ili kuweka mazingira wezeshi kwa wanawake na makundi mengine
kujumuishwa na kushiriki kikamilifu kugombea nafasi za uongozi  na vyombo va maamuzi katika ngazi mbalimbali.

 

·       Kuhamasisha vikundi vya kijamii (wanawake, wanaume, vijana,
wazee, watu wenye ulemavu) na Viongozi wa mila na dini ili kuwa mstari wa mbele
kutoa elimu na kuongeza uelewa kwenye jamii kuhusu haki za wajane kurithi na
kukemea ukatili na dhuluma za ndoa za utotoni na ukeketaji.

 

Katika siku ya tatu ya Tamasha,
washiriki waliandaa mikakati ya utekekelezaji wa mapendekezo yaliyoibuliwa
kutoka kwenye warsha kwa kuzingatia hali halisi kwenye kanda, rasilimali
zinazowazunguka na kwa kupitia nguvu za pamoja. Kwa namna ya kipekee, mikakati
hiyo imetambua umuhimu wa kushirikiana na viongozi wa mila, dini na wa Serikali
katika ngazi ya vijiji, kata na Halmashauri.

 

Katika namna iliyozidi kuheshimisha TGNP
kwa kuungwa mkono na Serikali, Mkuu wa Wilaya ya Same, Mheshimiwa Edward
Mpogolo atafunga Tamasha la Jinsia ya Kanda akiwa kama mwenyeji wa shughuli
zote zilifanyika kwa siku tatu.

Taarifa
hii imeandaliwa na:

Idara
ya Habari,

Ofisi
ya Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP

 

 

About the author

mzalendoeditor