Featured Kitaifa

SHAKA: ‘CCM ITASHIRIKIANA NA KILA MWENYE NIA NJEMA KWA MAENDELEO YA TANZANIA NA WATANZANIA’

Written by mzalendoeditor

 

Viongozi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Mkoa wa Dodoma (DWJ)  tarehe 28 Septemba, 2022 walimtembelea Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Itikadi na Uenezi Ndg Shaka Hamdu Shaka ofisini kwake Makao Makuu ya CCM Jijini Dodoma kwa lengo la kujitambulisha, kueleza kazi wanazozifanya na kuomba ushirikiano.

Shaka aliwahakikishia CCM wakati wote ipo tayari kushirikiana na yeyote au kikundi chochote chenye nia njema ya kuunga mkono juhudi za serikali katika kuharakisha maendeleo ya nchi yetu na watanzania kwa ujumla. Aidha aliwapongeza DWJ kwa kuijunga katika umoja na kufanya kazi za kurejesha kwa jamii huku akiwapa shime ya kutumia kalamu na taaluma zao kueleza mafanikio ya utendaji wa serikali ya CCM Awamu ya sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Nawapongeza kwa kujiunga katika umoja wenu pamoja na kazi mnazozifanya za kugusa maisha ya jamii hususani watu walio katika mazingira magumu kama vile mayatima, wagonjwa, wahitaji wengine pamoja na uhifadhi wa mazingira. Nawahakikishia CCM tutawaunga mkono. Ombi langu kwenu pamoja na kazi nzuri ya uandishi wa habari mnayoifanya nawaomba andikeni kuhusu kazi kubwa na nzuri inayofanywa na serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ili jamii ijue nini serikali yao inafanya na kuwanyima fursa wapotoshaji kupata himaya kwenye jamii yetu.” Alisema Shaka

Shaka alisisitiza kwamba ni vyema jamii yetu ikaunga mkono watu au vikundi vinavyojitoa kuunga mkono juhudi za serikali za kuharakisha maendeleo na kutoa huduma kwa jamii ili kuwatia moyo lakini pia ikiwa ni sadaka.

Kwa sasa DWJ inawahudumia wanafunzi watano wa kidato cha 5 na sita, inahudumia mwanamke mmoja mtu mzima mwenye tatizo la mifupa aliyelazwa taasisi ya mifupa Muhimbili (MOI) na wanatekeleza programu ya upandaji miti jiji la Dodoma.

About the author

mzalendoeditor