Featured Kitaifa

DIPLOMASIA YA KIUCHUMI YA RAIS SAMIA YAING’ARISHA TANZANIA YAPATA DOLA MIL 925 KUENDELEZA ELIMU-WAZIRI MKENDA

Written by mzalendoeditor

 

Na Mathias Canal, Kyela-Mbeya

Diplomasia ya kiuchumi iliyofanywa na inayoendelea kufanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan ndani na nje ya nchi imesaidia upatikanaji wa Dola za Marekani Milioni 925 kuboresha miundombinu ya elimu.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Prof Adolf Mkenda ameyasema hayo Wilayani Kela leo tarehe 7 Agosti 2022 wakati akitoa maelezo kuhusu sekta ya elimu kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa John Mwakangale wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan mkoani Mbeya.

Waziri Mkenda amesema kuwa Mradi huo utakaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano wa HEET ambao unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa gharama ya Dola za Marekani Milioni 425.0 sawa na shilingi bilioni 972.0 ambao ni Mkopo wenye masharti nafuu (concessional loan) kutoka Benki ya Dunia.

Prof Mkenda amesema kuwa lengo kuu la Mradi wa HEET ni kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, kuandaa mitaala mipya na kuboresha mitaala ya programu za kipaumbele ili iendane na mahitaji ya soko la ajira na kuimarisha mifumo ya usimamizi wa Elimu ya Juu nchini.

Mradi huo umebainisha Programu 14 za Fani za Vipaumbele vya Taifa ambazo ni pamoja na: Uhandisi na Teknolojia; TEHAMA; Malighafi Asilimia za Kisayansi; Sayansi ya Afya; Mipango Miji, Mazingira na Teknolojia; Nishati Jadidifu; Rasilimali Maji; Mabadiliko ya Tabia ya Nchi; Kilimo na Kilimo Biashara; Hifadhi ya Wanyapori; Utalii na Ukarimu; Taaluma ya Viwanda; Insia; na Ualimu.

Kadhalika, Waziri Mkenda amesema kuwa Dola Milioni 500 ni mradi wa kuimarisha ujifunzaji shule za msingi uliofadhiliwa na benki ya Dunia ambapo utekelezaji wa mradi huo wa miaka mitano utaboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji, ujuzi na ubora wa walimu katika ufunfishaji, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa rasilimali za utoaji huduma ngazi A halmashauri.

Kupitia mradi huo wa Boost shule 6000 nchi nzima zitatekeleza mpango wa shule salama, vituo vya walimu na shule za msingi 800 kiwekewa vifaa vya TEHAMA kwaajili ya kuwawezesha walimu kujifunza na utoaji wa mafunzo endelevu kwa walimu, madarasa 12000 ya Elimu ya awali kuboresha, uandikisha wa wanafunzi elimu ya awali kuongezeka.

Pia, Waziri Mkenda amesema kuwa Rais Samia amekusudia kuboresha sekta ya elimu na kupitia uongozi wake ulio bora ni wazi kuwa kwenye sekta ya elimu Yajayo yanafurahisha.

About the author

mzalendoeditor