Featured Makala

SERIKALI KUWEKEZA NGUVU ZAIDI KATIKA KUPAMBANA NA MADAWA YA KULEVYA

Written by mzalendoeditor

 

WAZIRI  wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. George Simbachawene,akizungumza na waandishi wa habari   wakati  akielezea vipaumbele vya bajeti  katika Wizara hiyo na taasisi zilizochini yake kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

…………………………………………

Na Alex Sonna– Dodoma.

Serikali imesema itawekeza nguvu zaidi katika kupambana na madawa ya kulevya ambapo zaidi ya shilingi bilioni 11.9  zimeidhinishwa  katika mwaka wa fedha 2022/23 kwa Mamlaka ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya Nchini kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake ukilinganisha na kiasi cha Shilingi bilioni 8.5 kilichoidhinishwa mwaka wa fedha 2021/22 sawa na ongezeko la asilimia 28.8.

Hayo yamebainishwa leo Julai 29,2022 Jijini Dodoma na Waziri  wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. George Simbachawene  wakati akielezea vipaumbele vya bajeti  katika Wizara hiyo na taasisi zilizochini yake kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Ambapo amesema ongezeko hilo la bajeti ya mamlaka hiyo litaendelea kuimarisha udhibiti wa biashara na matumizi ya dawa za kulevya nchini, kuimarisha ushirikiano miongoni mwa vyombo vinavyojihusisha na udhibiti wa dawa za kulevya kitaifa na kimataifa.

Mhe. Simbachawene amesema kuwa fedha hizo zitatumika katika kubadilishana taarifa na kuimarisha ukusanyaji wa taarifa za kiintelijensia zinazohusu biashara haramu ya Dawa za kulevya na kuendesha operesheni za pamoja.

“Ofisi itaboresha huduma za tiba kwa waathirika wa dawa za kulevya kwa kuongeza idadi ya vituo vya tiba na urekebishaji wa tabia ya waathirika wa Dawa za Kulevya nchini” amesema Simbachawene

Ameongeza kuwa  “pamoja na kuweka programu maalum ya elimu ya maisha (Life skills) na mafunzo ya ufundi pamoja na kuwapatia vifaa (startup kits) ili waweze kuajiriwa au kujiajiri na hivyo kuwa na shughuli za kiuchumi za kufanya” amesema

Mhe.Simbachawene amesema kwa upande wa Tume ya kudhibiti UKIMWI Tanzania imeidhinishiwa na Bunge zaidi ya Shilingi bilioni 14.9 ambapo zaidi ya shilingi bilioni 2.9 ni kwa ajili ya matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni 12.0 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ukiilinganisha na bajeti ya Shilingi bilioni 3.17 zilizotengwa mwaka 2021/22 kwa ajili ya kutekeleza shughuli za matumizi ya kawaida na maendeleo sawa na ongezeko la asilimia 71.2.

Amesema kuwa shughuli zitakazotekelezwa kwa mwaka wa fedha 2022/23 ni pamoja na kuratibu upatikanaji wa huduma za VVU na UKIMWI kwenye Mikoa ya kipaumbele ikiwemo; Iringa, Kagera, Katavi, Mbeya, Mwanza, Njombe, Pwani, Ruvuma, Shinyanga, Dodoma, Geita, Tabora na Songwe pamoja na kuweka kipaumbele katika kuzuia maambukizi ya VVU kwa vijana wa miaka 15 – 24.

Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2022/2023 imeidhinishiwa zaidi ya shilingi 101,030,914,000 kwa ajili ya matumizi kati ya fedha hizo shilingi bilioni 15.74 ni mishahara, bilioni  47.85 ni matumizi mengineyo na bilioni 17.56 ni ruzuku kwa vyama vya siasa na bilioni 19.87 ni katika miradi ya maendeleo.

Amesema bajeti hii ni sawa na ongezeko lazaidi ya asilimia 20.61 ukilinganisha na bajeti ya shilingi bilioni 80.17 iliyotengwa kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

About the author

mzalendoeditor