Featured Kitaifa

MAKATIBU WAKUU WANAOSIMAMIA SEKTA MBALIMBALI WA NCHI ZA EAC WAKUTANA JIJINI ARUSHA

Written by mzalendoeditor

Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ukiendelea jijini Arusha.

Meza Kuu kutoka kulia ni; Bw. Severin Mbarubukeye Katibu Mkuu anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki, Vijana Michezo na Utamaduni kutoka Burundi,  Bi. Edith Mwanje Katibu Mkuu Wizara ya Afrika Mashariki kutoka Uganda, Bw. Saitoti Torume CBS, Katibu Mkuu wa Hazina na Mipango kutoka Kenya, Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Bw. Adrea Aguer Ariik Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afrika Mashariki ya Jamhuri ya Sudan Kusini.

…………………………………………

Mkutano wa 42 wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika ngazi ya Makatibu Wakuu umefanyika leo tarehe 11 Juni 2022 katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha.

Mkutano huo ambao umetanguliwa na mkutano wa Maafisa Waandamizi uliofanyika tarehe 8 na 9 Juni 2022 ulikuwa jukumu maalumu la kupokea na kupitia taarifa, agenda na mapendekezo yaliyotokana na Mkutano wa Maafisa Waandamizi kuhusu masuala mbalimbali ya Jumuiya na hatimaye, kuyawasilisha katika Mkutano wa Mawaziri utakaopangwa kufanyika baadaye mwaka huu. 

Miongoni mwa masuala yaliyojiri katika mkutano huo ni uzingatiwaji wa ripoti mbalimbali ikiwemo ripoti ya kutoa mwelekeo wa kuanza kutumika kwa lugha ya Kifaransa na Kiswahili katika uendeshaji wa shughuli za kiofisi/rasmi za Jumuiya. 

Katika Mkutano huo ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Faraji Kasidi Mnyepe

Viongozi wengine walioambatana naye ni pamoja na, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo, Katibu Mkuu Afisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji –Zanzibar Bi. Khadija Rajab Khamis, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Kh. Shaaban, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Mweli na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi Umma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi. Wengine waliombatana naye ni Balozi Stephen P. Mbundi Mkurugenzi wa Siasa, Ulinzi na Usalama, Bw. Bernard Haule Mkurugenzi Biashara, Uwek ezaji na Sekta za Uzalishaji na Bw. Eliabi Chodota, Mkurugenzi Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii, wote wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na Maafisa kutoka Wizara mbalimbali. 

Mkutano huo uliofanyika kwa njia mseto (video na ana kwa ana) umehudhuriwa na nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mwenyekiti wake Bw. Saitoti Torume CBS ambaye ni Katibu Mkuu wa Hazina na Mipango kutoka Jamhuri ya Kenya 

Baraza la Mawaziri ni chombo cha kutunga sera za Jumuiya. Baraza hilo linajumuisha Mawaziri wanaosimamia Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki au Ushirikiano wa Kikanda.

Miongoni mwa majukumu ya Baraza la Mawaziri la Jumuiya ni kufuatilia na kufanya mapitio ya mara kwa mara juu ya utekelezaji wa programu za Jumuiya na kuhakikisha utendaji kazi mzuri wa Jumuiya.

About the author

mzalendoeditor