Featured Kitaifa

WANASHERIA SEKTA YA MAJI WATAKIWA KWENDA NA KASI YA MAGEUZI  YA KISEKTA

Written by mzalendoeditor

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso akizungumza na Wanasheria wa Sekta ya Maji katika kikao kazi cha wanasheria wote wa sekta hiyo mkoani Morogoro.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso (kulia) akiwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Sheria Wizara ya Maji, Simon Nkanyemka katika kikao kazi cha Wanasheria wa Sekta ya Maji mkoani Morogoro.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Wizara ya Maji, Barnabas Ndunguru akitoa mada kuhusu Maadili ya Utumishi wa Umma katika katika kikao kazi cha Wanasheria wa Sekta ya Maji mkoani Morogoro.

Baadhi ya Wanasheria wa Sekta ya Maji kutoka Wizara ya Maji na taasisi zake wakiwa katika kikao kazi mkoani Morogoro.

Mgeni Rasmi Waziri wa Maji, Jumaa Aweso akiwa na wajumbe wa meza kuu katika kikao kazi cha Wanasheria wa Sekta ya Maji mkoani Morogoro.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso akiwa kwenye picha ya pamoja na Wanasheria wa Sekta ya Maji katika kikao kazi  mkoani Morogoro.

……………………………………….

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amewataka Wataalam wa Sheria wa Sekta ya Maji kuzipitia upya sheria za maji na kuziboresha ikibidi ili kuendana na kasi ya mageuzi ya kisekta.

Ametoa rai hiyo wakati akifungua kikao kazi cha siku tatu cha Wanasheria wa Sekta ya Maji mkoani Morogoro.

Waziri Aweso amesema mabadiliko na mageuzi makubwa yanayoendelea  kwenye Sekta ya Maji yanahitaji Wanasheria kujituma zaidi na kuongeza ufanisi kwenye majukumu yao, huku akiwataka kuzijua vizuri sheria pamoja na kuzitafsiri kwa mustkabali wa sekta.

Akisema kuwa zipo changamoto mbalimbali katika Sekta ya Maji ikiwa ni pamoja na upotevu wa maji unaochangiwa na wizi wa maji, uharibifu wa miundombinu ya maji na usimamizi mzuri wa mikataba ya miradi mbalimbali na kuzingatia thamani ya fedha.

Waziri Aweso amesema Wanasheria wana mchango muhimu sana katika kufanikisha malengo ya Sekta ya Maji  katika kuepusha na kutatua migogoro ya kiutumishi, utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma.

Aidha, Waziri Aweso amesema kwa sasa Sekta ya Maji ina Wanasheria 55 ambao wameajiriwa na wizara na taasisi 23 tu zilizo chini ya wizara na kuzielekeza taasisi zote kuweka na kutekeleza mipango ya kuajiri wanasheria wenye sifa na weledi ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya kisheria kwa ufanisi.

Awali, Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Sheria Wizara ya Maji, Simon Nkanyemka amesema malengo ya kikao ni kufahamiana, kubadilishana uzoefu na mbinu za kikazi pamoha na kuongezeana uwezo katika maeneo mbalimbali ya kitaalam na kiutumishi.

Akisema kuwa kikao hicho ni cha pili mara baada ya kikao cha kwanza kilichofanyika Septemba, 2018 ambacho pamoja na masuala mbalimbali kilipitia na kutoa maoni kuhusu mapendekezo ya kutungwa kwa Sheria ya Huduma za Maji na Usafi wa Mazingira Na. 5/2019  ambayo inatumika sasa.

About the author

mzalendoeditor