Featured Kitaifa

ZUNGU ATETA NA RAIS MWENZA WA BUNGE LA UMOJA WA ULAYA

Written by mzalendoeditor

Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Bunge la Umoja wa Ulaya yamekubaliana kuimarisha
ushirikiano miongoni mwao na miongoni mwa wabunge wao. Hayo yameafikiwa tarehe 02
Aprili 2022 kwenye makao makuu ya Bunge la Umoja wa Ulaya nchini Ufaransa, wakati
wa mazungumzo baina ya Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Mussa Azzan Zungu na  Rais mwenza wa
Bunge la Pamoja la Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Nchi za Afrika, Caribbean na
Pasifiki (OACPS), Mhe. Prof. Carlos Zorrinho). 

Mazungumzo hayo yaliyofanyika
pembezoni mwa Mkutano wa 41 wa Bunge  la
OACPS na EU  ambapo Mhe. Zungu anaongoza
ujumbe wa Tanzania, viongozi hao walikubaliana pia kupitia Mabunge yao
kuhakikisha kuwa uhusiano mzuri uliopo baina ya Tanzania na Umoja wa Ulaya na baina
ya Bunge la Tanzania na Bunge la Umoja
wa Ulaya unaimarishwa zaidi.

Aidha, Mhe. Zungu alitumia fursa
hiyo kumwalika Mhe. Zorrinho pamoja na  baadhi ya Wabunge wa Bunge la EU kuitembelea
Tanzania na kujionea wenyewe hatua mbalimbali zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suhuhu Hassan katika kusukuma maendeleo ya
Tanzania. Rais huyo mwenza wa Bunge la Pamoja la Ulaya na ACP alipokea mwaliko
huo kwa furaha  na kuahidi kufanya ziara
hiyo nchini siku zijazo akiambatana na baadhi wa Wabunge wa Bunge la Umoja wa
Ulaya. Alieleza kuwa Tanzania ni moja ya nchi za kipaumbele kwa Umoja wa Ulaya
na Bunge hilo linafurahishwa na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Tanzania kusimamia
ajenda za maendeleo na ustawi wa jamii, hususan katika kuboresha mazingira ya
uwekezaji na kuimarisha demokrasia na haki za binadamu.

Mhe. Zungu alimwomba
mwenyeji wake huyo kuwahamasisha wawekezaji wa Ulaya waendelee kuja kuwekeza
nchini kwenye masuala ya uchimbaji wa gesi na maeneo mengine, kwani Tanzania imebarikiwa
kuwa na fursa nyingi za uwekezaji.

Viongozi hao walihitimisha mazungumzo
yao kwa kusisitiza umuhimu wa kuongeza ushawishi wa mabunge yao kutoa miongozo
itakayoimarisha ushirikiano baina ya Umoja wa Ulaya na nchi za Afrika,
Carribean na Pacific pamoja na masuala yanayohusu kukabiliana na mabadiliko ya
tabianchi na kuimarisha amani eneo la ukanda wa maziwa makuu hususan nchini
Msumbiji. Professa Zorrinho alieleza kuwa EU ina imani kubwa zaidi na Tanznaia
katika masuala ya usuluhishi wa migogoro na kukuza amani duniani.

Katika
mazungumzo hayo, Mhe. Zungu aliambatana na Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji
na kwenye Umoja wa Ulaya, Mhe. Jestas Abuok Nyamanga na maafisa wengine
waandamizi wa Ubalozi na Bunge.

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Assan Zungu  (kushoto) akisalimiana na Mhe. Professa Carlos Zorrinho, Rais mwenza
wa Bunge la Pamoja la OACPS na EU (kulia) wakati wa kikao chao kilichofanyika
katika ofisi za Bunge la EU zilizopo Strasbourg,Ufaransa. Tukio hilo
lilifanyika tarehe 02 Aprili,2022 wakati wa Mkutano wa Bunge la Pamoja la OACPS
na EU unaoendelea Strassbourg.

 Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Mussa Assan Zungu (aliyesimama) akichangia katika moja ya kikao cha Bunge la Pamoja la
OACPS na EU kilichofanyika katika ofisi za Bunge la EU zilizopo
Strasbourg, Ufaransa. Tukio hilo lilifanyika tarehe 02 Aprili, 2022. Mhe.Zungu
analiwakilisha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vikao hivyo.

 

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Assan Zungu  (katikati kulia) akiwa katika kikao chake na Mhe. Professa Carlos
Zorrinho, Rais mwenza (co-President) wa Bunge la Pamoja la OACPS na EU (wa pili
kushoto) wakati wa kikao chao kilichofanyika katika ofisi za Bunge la EU zilizopo
Strasbourg,Ufaransa. Tukio hilo lilifanyika tarehe 02 Aprili, 2022 wakati wa
Mkutano wa Bunge la Pamoja la OACPS na EU unaoendelea Strasbourg. Kulia mwa
Mhe. Zungu ni Mhe. Jestas Nyamanga, Balozi wa Ubalozi wa Jamhuri wa Muungano
nchini Ubelgiji na kwenye Umoja wa Ulaya (kulia) na maofisa wengine kutoka
Bunge la Tanzania na Bunge la EU.

 

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, 
Mhe. Mussa Assan Zungu,  (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Balozi Dkt George Pinto
Chikoti, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya OACPS (kulia) na Mhe Balozi Jestas Abuok
Nyamnaga (kushoto) nje ya ukumbi kunakofanyika Mkutano wa 60 wa Bunge la OACPS
unaofanyika katika ofisi za Bunge la EU jijini Strasbourg, Ufaransa. Tukio hilo
lilifanyika tarehe 29 Machi, 2022. Mhe. Zungu analiwakilisha Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania katika vikao hivyo.

 

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Mussa Assan Zungu  (aliyesimama kulia) akibadilishana mawazo na mmoja wa Wabunge wa Bunge
la Umoja wa Ulaya wakati wa Mkutano wa 41 wa Bunge la Pamoja la OACPS na EU uliofanyika katika ofisi za Bunge la EU zilizopo Strasbourg,Ufaransa. Tukio
hilo lilifanyika tarehe 02 Aprili, 2022. Mhe. Zungu analiwakilisha Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vikao hivyo.

 

About the author

mzalendoeditor